STORY-PENZI LA MSHUMAA
MTUNZI-MZIRAY F.M.
SEHEMU YA 8
Ilipoishia sehemu ya 7
“Sikilizeni niwaambie,suala la dini haliwezi kupima upendo alionao mtu kwa mchumba wake.Mnaweza mkaoana watu wa dini moja na msielewane.Au kama mnaona hiyo ni mbaya mimi nipo tayari kubadilisha dini ili tuwe kitu kimoja.”
“Aaaaah!hapana mwanangu huko umefika mbali sana.Endelea tu na hiyo ndoa yako ya mahakamani haina neno.Mbona watu wanaoana kimila mabomani huko na ndoa zao zinakuwa vizuri tu.Mwanangu Denis,sasa hivi sitaki kukubugdhi hata kidogo.Fanya maamuzi yako mwenyewe.Kile unachoona ni sahihi na kitafurahisha moyo wako kifuate hicho hicho.Sitaki baadae upate matatizo halafu utusingizie sisi.Mimi sina tena neno na wewe,nakupa baraka zote katika ndoa yako na ninakutakia maisha mema.”Mzee Mwamba aliamua kumuunga mkono mwanaye Denis baada ya jitihada zake za kutaka kumzuia asimuoe Shaimaa kushindikana.
“Asante sana baba yangu.Nashukuru mno kwa uelewa wako.”Denis aliinuka kwa shangwe na kumkumbatia baba yake kwa furaha.
“Baba.”Brenda aliita kwa unyonge.
“Nini!Unataka kuleta umbea siyo?”Denis alimgeukia Brenda na kumpaka.
“Hebu huko,sijakuita wewe!”Brenda alijibu kwa jeuri.
“Ehe!unasemaje?”Mzee Mwamba aliuliza baada ya kuachiana na Denis.
“Yaani umekubali kaka Denis amuoe huyo shangingi wake wa Kitanga?”
“Brenda usinitafute,nani shangingi?Nitakubomoa sasa hivi.”Denis alikasirishwa sana na maneno ya shombo toka kwa mdogo wake.
“Brenda funga huo mdomo wako.Shenzi kabisa.Ujue huyu ni kaka yako hivyo unapaswa kumheshimu.Pumbavu!Hayawani mkubwa wewe.”Mzee Mwamba alifoka kwa sauti ya ukali.Brenda aliamua kukiacha kikao kile na kuingia zake chumbani.
“Mmmh!huyu ana kisirani gani?”Bi Asma aliuliza kwa masikitiko baada ya binti yake kuondoka.
“Kwahiyo mama na wewe umekubaliana na maamuzi ya baba?”Winfrida alimtupia mama yake swali hilo huku akiwa na kimuhemuhe cha hali ya juu.
“Winfrida jichunge,utamfuata Brenda sasa hivi.”Denis aliingilia kati.
“Mbona una kiherehere sana.Kwanini mimi nimekuuliza wewe?”Winfrida alimzodoa kaka yake.
“Hivi mbona mnanifuatilia sana au mnataka niwaoe nyie?”Denis alifoka.
“Heeeh!Denis maneno gani hayo unayomwambia dada yako?Kwahiyo wasikuambie ukweli au?Mimi mwenyewe sijakubaliana na nyie hata kidogo.Hivi baba Denis unaona ni sahihi kabisa Denis amuoe huyo mwanamke aliyetaka kumtoa roho kwa mawazo?”Bi Asma hakukubaliana hata chembe juu ya uamuzi alioutoa mume wake.Yeye pamoja na mabinti zake hawakutaka hata kumsikia Shaimaa sembuse kumuona!
“Mwambie huyo mama.”Winfrida alishadadia.
“We koma,tena ukome na ukomae.Shika adabu yako,kiroboto mkubwa wewe.Kama unashindwa kuzungumza maneno yenye busara mfuate mwenzio chumbani.Shenzi kabisa.Hivi ninyi wanawake huwa mna akili za aina gani?”Mzee Mwamba hakutaka mzaha hata kidogo.
“Kwahiyo mimi na wanangu tupo sawa?”Bi Asma hakufurahishwa na kauli ya mumewe.
“Sikuwa na maana hiyo mke wangu.”Mzee Mwamba alijitetea.
“Hukuwa na maana hiyo!Ulikuwa unamaanisha nini?Eti hizi akili za wanawake ni za aina gani?Ni za aina hiyo hiyo unayoifahamu wewe.Kifupi ni kwamba simtaki huyo mchumba wa Denis.Kama ameachana na Vivian amtafute mwanamke mwingine.”Mama yake Denis alichafukwa kisawasawa.
“Mtafutie basi wewe.”Mzee Mwamba aliropoka.
“Nimtafutie mimi!kwani yeye ni bubu au kipofu?Halafu baba Denis mbona unanikosea heshima hapa mbele ya watoto?Hivi ni picha gani tunayoitengeneza hapa?”Bi Asma aalizidi kufoka kwa hasira.
“Iwe picha ya Kihindi au ya Kizungu utajua mwenyewe.Mwanangu Denis,oa mwanamke yeyote unayemtaka mimi nipo nyuma yako.”
“Aoe mwanamke yeyote anayemtaka eeh!”
“Eeeh.”
“Wewe si ndiyo ulikuwa mstari wa mbele kulipinga hili suala la Denis kumuoa huyo binti wa Kitanga?”Bi Asma alimtazama mumewe na kumtwanga swali hilo kwa ukali.
“Nilikuwa namwonea tu bure.Kwani mimi nililazimishwa kukuoa wewe?Si nilikuchagua mwenyewe.Wewe ungelazimishwa ungekubali?”Bi Asma aliishiwa pozi baada ya mumewe kumhama na kuhamia upande wa pili wa mwanaye.Denis alifurahi sana kuungwa mkono na baba yake.Aliamini kuwa kama Mzee Mwamba yupo pamoja na yeye hata hao wengine wakigoma haina shida.Ilimradi tu amepata baraka angalau za mzazi mmoja kila kitu kitakwenda kama kilivyopangwa.Bi Asma alimshika bintiye mkono haoo wakaingia zao chumbani na kuacha kikao kikitawaliwa na chips dume.
“Hivi kwanini mama anapinga mimi kumuoa Shaimaa?”Denis aliuliza kwa unyonge.

“Achana na hayo mambo.Hilo suala niachie mimi wala usiwe na wasiwasi.Najua nitazungumza naye vipi mpaka akubaliane na hali halisi.We endelea na hiyo mipango yako,kila kitu kitakuwa sawa.Vipi kuhusu suala la mahari,tunapeleka lini?Usije ukamchukua binti wa watu bila wazazi wake kufahamu!”Kweli Mzee Mwamba alidhamiria kuwa bega kwa bega na mwanaye.
“Kuhusu suala la mahari baba nilishamalizana nalo muda mrefu.Niliongea na baadhi ya wazee ambao ni marafiki zangu wakaenda ukweni kumalizana nao.Niliamua kufanya hivyo kwasababu ninyi mlishaonesha kunitenga tangu mwanzoni kabisa.”Denis alizungumza huku akiwa kayatupa macho yake pembeni kwa aibu kutokana na kitendo alichokifanya.
“Daah!mwanangu Denis,kwanini ulichukua maamuzi ya haraka kiasi hicho?Umetudhalilisha sana sisi wazazi wako.Sasa siku hiyo utatutambulishaje mbele ya wazee wenzetu?”Mzee Mwamba alisikitishwa mno na maelezo ya Denis.
“Sasa baba unafikiri mimi ningefanyaje?Ninyi ndiyo mna makosa na mnastahili kulaumiwa.Mmengekubali tangu mwanzoni kuwa upande wangu haya yote yasingetokea.”Denis alimshushia baba yake zigo za lawama.
“Utusamehe sana mwanangu.Nilikuwa nang’ang’ania kitu ambacho kingepoteza furaha yako.Hiyo haina shida,tutajua namna ya kuzungumza nao.Kwahiyo maandalizi ya harusi yanaendeleaje?Nimesikia ukisema kuwa uhitaji kamati ya harusi sasa sijui hiyo sherehe yako itakuaje?”Mzee Mwamba alitaka kujua kinachoendelea ilimradi kufanikisha tukio hilo.
“Mimi sifanyi sherehe ya kualika Tanzania nzima.Nafanya katafrija kadogo tu cha kishkaji ambayo itaudhuriwa na watu wachache mno.Sitaki kuonekana mtu wa fahari sana ndiyo maana nimeamua kufanya hivyo.”Denis alimfafanulia baba yake namna mambo yalivyopangwa katika sherehe yake.
“Ni vizuri,mimi siwezi kuingilia.Kwahiyo ni siku gani unatarajia kufunga hiyo ndoa yako?”Mzee Mwamba alitaka kujua siku ya harusi hiyo.
“Nimepanga kufunga ndoa siku ya Ijumaa katika mahakama ndogo ya Wilaya ya Mkuranga.”
“Haaa!kwahiyo umeamua kufungia huko huko Mkuranga kwako unapokaa?”
“Ndiyo hivyo mzee,au wewe unataka nifungie wapi?”
“Aaah!mimi sina neno.Popote unapoona ni sahihi wewe kamilisha tu mambo yako.”
“Nashukuru sana baba kwa kuniunga mkono.Ngoja nikakuchukulie mzigo kidogo kwaajili ya kununulia nguo za sherehe hiyo.”
Denis alitoka nje na kufungua mlango wa nyuma wa gari lake na kuibuka na brufkesi ndogo.Baada ya hapo alifunga mlango wa gari na kuingia ndani ya nyumba yao. “Humo katika hilo begi kuna kama milioni tano hivi.Mtatumia hizo pesa kununulia nguo na kama hazitawatosha utanipigia simu niwaongezee.”
Denis alimkabidhi baba yake zile pesa na kumpatia maelekezo ya matumuzi yake. “Nashukuru sana mwanangu.Hizi pesa ni nyingi sana wala hazihitaji nyongeza yoyote ile.”Mzee alitoa shukrani zake kwa mwanaye huyo aliyekuwa na utajiri wa hali ya juu.
“Usiogope kutumia pesa zangu.Haya ndiyo matunda ya kuza dume la mbegu baba.Mkanunue nguo zinazoendana na hadhi yenu.Sitaki kuwaona mkiwa mmevaa nguo za ajabu ajabu katika sherehe yangu.Mtaenda na Brenda,yeye anafahamu maduka yenye nguo nzuri hapa mjini.Mimi ningekuwa na nafasi ningewapeleka lakini nina mambo mengi mno ya kufanya.”Denis alimtaka baba yake awe huru katika matumizi ya pesa zake.
“Usijali mwanangu,kila kitu kitakwenda kama kilivyopangwa.”
“Baba ngoja sisi tuondoke kwasababu kuna sehemu tunataka tupitie.Nafikiri naweza nikaja huku kesho ama keshokutwa kuwajulia hali.”
“Haya mwanangu,Mungu akutangulie katika mambo yako.Ila nasikitika mnaondoka kama mlivyokuja.Wadogo zako bado hawajapika chai.Walipoamka tu wakakutana na ugeni wa Vivian ndiyo tukaingia kikaangoni.Sasa hivi naona wameenda kujivundika ndani.”
“Aaah!usijali mzee,sisi tupo kamili gado.Utatusaidia kumuaga mama pamoja na akina Brenda.Nadhani sasa hivi bado wamechafukwa kutokana na hili lililotokea hapa.”
“Ha!ha!ha!ha!we nenda baba mimi najua namna ya kuzungumza na mama yako naye akazungumza na wanaye.Kila kitu kitakwenda sawa.”Mzee Mwamba alimtia mwanaye moyo na kumtakia kila la heri katika kufanikisha mambo yake.
“Haya baba kwaheri.”
“Haya mwanangu,endelea kuzitunza busara ulizokuwa nazo.”
“Ha!ha!ha!ha!nyie wazee wetu ndiyo mna busara na hekima kushinda sisi.”Dick alipoaga,Mzee Mwamba hakusita kumsifia kutokana na maneno yake ya busara aliyoyatoa katika kikao kile.Walipofika nje Denis alimrukia rafiki yake kwa furaha nusura ambwage chini.
“Yes!mambo si ndiyo hayo.”
“Vipi Denis,mbona una furaha namna hiyo?”Dick aliuliza kwa mshangao.
“Ujue wewe ndiyo umesababisha baba abadilishe mawazo.”Denis aliongea huku akiongoza njia kulifuata gari.
“Kivipi?”Dick alipouliza swali hilo,Denis aliacha kufungua mlango wa gari na kumgeukia.
“Unaniuliza kivipi tena?”
“Ndiyo.”

“We unadhani maneno uliyoongea pale ni ya kitoto?Yaani umemkamata baba kisawasawa.Mimi namfahamu Mzee Mwamba akishikilia jambo hata kama ni la kijinga hawezi kubadili msimamo wake kirahisi namna hiyo.Lakini wewe umemuweza kweli kweli.Ujue sikuamini pale baba alipoanza kuzungumza kwa upole baada ya wewe kutema cheche zako.Kwa jinsi alivyokuwa anaongea nikajua hapa kwisha habari yake.”Denis alimsifia rafiki yake kwa jinsi alivyozungumza maneno ya busara na kuulainisha moyo wa  Mzee Mwamba ambapo aliamua kumwacha mwanaye afanye maamuzi yake mwenyewe.

                                                              ********
Itaendelea.....Nashukuru kwa ufuatiliaji wako wa hadithi hii naamini utajifunza mengi na utaburudika.Nakutakia siku njema na Mungu akubariki.
                                                            *******
Kw amaoni au ushauri napatiana kwa namba 0655089197/0766123623

Share this

Related Posts

Previous
Next Post »

2 comments

comments
31 July 2016 at 03:42 delete

Kama kawaida...hadithi tamu za kumwaga ndani ya nyumba

Reply
avatar
31 July 2016 at 03:42 delete

Kama kawaida...hadithi tamu za kumwaga ndani ya nyumba

Reply
avatar