STORY-PENZI LA MSHUMAA
MTUNZI-MZIRAY F.M.
SEHEMU YA 19
Ilipoishia sehemu ya 18
Tangu wazaliwe hawajawahi kuingia katika hoteli ya kisasa kama hiyo na kupata msosi wa namna ya kipekee.Muda wote walikuwa wanashangaashangaa kama vile wapo feri.Baada ya kumaliza kupata kifungua kinywa Denis aliwaingiza wazee wale ndani ya gari lake na kuanza safari ya kuelekea nyumbani kwao katika kata ya Chumbageni maeneo ya Kisosora.Walipita kwenye mzunguko wa pale Kwaminchi na kunyoosha barabara ambapo baada ya kuuvuka msikiti walikata kushoto na kuendelea na safari.

Sasa endelea....
Denis aliendelea kuionea lami kwa kukanyaga mafuta mpaka alipoiacha barabara inayoelekea Ikulu ndogo na kukata kulia.Hapo ndipo walipoingia rasmi mtaa wa Kisosora ambapo kutokana na maelezo ya wazee wale Denis alifanikiwa kupaki gari mbele ya nyumba yao.Nyumba ya familia hiyo ilikuwa ni ya udongo lakini ilipigwa plasta kwa nje na kupakwa rangi.Juu iliezekwa kwa makuti na iliegemea upande mmoja kuashiria kuwa muda wowote ingeweza kuanguka.
Denis alikaribishwa stuli na kuketi pale barazani.Aliendelea kuyashibisha macho yake kwa kuangaza huku na huko akiyasawiri vizuri mazingira yale.Watu wengi wa mtaa ule walitoka na kujipitisha katika nyumba ile ili wajue ni nani aliyekuja na gari la kisasa namna ile.Denis alizungumza mambo mengi sana na wale wazee ikiwemo kuwasaidia kuboresha mazingira yao ya kuishi.Bi Zena na mumewe walifurahi sana na kuanza kujichekesha kwa aibu baada ya kumkashfu mno kijana huyo.
“Tunashukuru sana kijana wetu,Mungu akubariki na akuzidishie.”
“Asante sana baba kwa ahadi yako.”
“Msijali wazee wangu,haya ni mambo ya kawaida.Mimi ngoja niwaache kuna mambo yangu nataka nikayafuatilie halafu jioni nitakwenda hospitali kumjulia hali Shaimaa sambamba na kumpelekea chakula.”
“Hamna tatizo,ubarikiwe sana baba.”
“Chukueni hiki kiasi kidogo cha fedha kitawasaidia siku mbili tatu.Kesho nitakuja asubuhi kuwachukua mkamwone mtoto wenu.Vile vile tutapanga namna ya kusafiri naye kuelekea Dar-es-salaam.”
“Haya mwanangu,asante sana baba.”Denis aliagana na wale wazee kisha akaenda shughuli zake zilizompeleka Tanga.Angalau furaha ilirejea katika familia ya Mzee Kambi.Kitita cha pesa walichoachiwa na Denis kiliwapagawisha mno.Siku hiyo hawakunywa pombe ya mnazi,badala yake walienda kukata bia mpaka jioni.Walirejea nyumbani wakiwa bwi!Waliwakuta wajukuu wao wakipiga miayo kwa njaa.
Bi Zena alitoa noti ya shilingi kumi na kuwapa mabinti hao na kuwaambia wakale chochote wanachokitaka.Wasichana hao walishangaa sana kwani haijawahi kutokea hata siku moja wazee hao wakawapa pesa ya matumizi.Asubuhi wakati Denis alipokwenda katika nyumba hiyo,wao walikuwa wamekwenda shuleni.
Siku iliyofuata asubuhi na mapema Denis kama alivyoahidi aliwafuata Mzee Kambi na mkewe wakaelekea Bombo hospitali ambayo ni hospitali ya mkoa wa Tanga.Walifanikiwa kumwona Shaimaa ambaye bado hali yake haikuridhisha hata kidogo.
Walihuzunika sana lakini ndani ya nyoyo zao kulijaa tumaini la kupona kwa binti yao baada ya mipango yote ya safari ya kumhamihsia Muhimbili hospitali kukamilika.Wazazi wa Shaimaa walimshangaza sana Denis kwa kumwambia kuwa yeye aondoke na Shaimaa peke yake kwasababu wao watabaki kuwaangalia wale mabinti wanaosoma.Kilichomfanya Denis ashangae zaidi ni namna wazee hao walivyomwamini haraka namna hiyo wakati siku kadhaa zilizopita walikuwa wakali kama Mbogo aliyejeruhiwa.
“Yaani anayeumwa ni binti yao halafu wananiambia niondoke naye mimi mwenyewe bila wao kuwepo!Mmmh!wana lengo gani na mimi?Inamaana hawana ndugu yeyote atakayebaki na hao watoto?Kwanza mbona wanaonekana ni mabinti wakubwa tu!”Denis aliamua kuzungumza na Mzee Kambi ili angalau yeye aende naye halafu mkewe abaki kuangalia familia.
“Hapana kijana ni bora mke wangu aende maana yeye ndiyo ataweza kumhudumia binti yake.Mimi nitabaki nyumbani na hawa watoto wala hamna tatizo.”Mzee Kambi alijitoa kwenye mpango wa kwenda Dar-es-salaam.
“Ni kweli kabisa hilo ni wazo zuri.Mama,itabidi tusafiri wote.”Denis alilikubali wazo la Mzee Kambi na kuona kuwa kuna umuhimu wa kwenda na mama mtu akamuuguze mwanaye.Ilibidi atumie nguvu ya ziada kumshawishi mama huyo akubali kwenda kumhudumia mwanaye atakapokuwa hospitali.Sababu kubwa iliyokuwa inawafanya wazee hao wawe wagumu kwenda Dar-es-salaam ni kuhofia kuzikosa starehe wanazozifanya pale Tanga.
Ni jambo la kushangaza sana kwa wazazi kukwepa kwenda kuuguza binti yao eti kisa starehe zisizokuwa na misingi yoyote na kumwachia mzigo wote mtu ambaye hausiki kabisa na familia ile.Baada ya Denis kusisitiza sana ilibidi Bi Zena akubali kwa shingo upande.Walipotoka pale Bombo hospitali walielekea kituo cha polisi Raskazoni kufuata vitambulisho vya Denis.Wazazi wa Shaimaa waliomba kesi hiyo ifutwe baada ya Denis kuonesha moyo wa kuwasaidia kwa hali na mali.
Hata hivyo pesa za kuifuta kesi hiyo alizotoa Denis mwenyewe kwa kuwa alikuwa anataka vitambulisho vyake.Baada ya kutoa fedha alipewa vitu vyake sambamba na kitambulisho cha Dick alichokiacha kama mtoa dhamana wa Denis.Walipotoka hapo walipitia hotelini na kupata chakula kisha Denis akawarudisha wazee hao nyumbani kwao na kumwambia Bi Zena ajiandae kwa safari ya siku inayofuata.Denis hakutaka kumwambia mtu yeyote kuwa anarejea Dar-es-salaam kesho yake.Aliamua kufanya hivyo ili kuwashtukiza wazazi wake pindi atakapokwenda kuwajulia hali.
Palipopambazuka tu Denis alienda kukabidhi funguo wa chumba pale mapokezi na kuwashukuru kwa huduma nzuri waliompatia.Yule dada wa mapokezi naye hakusita kumshukuru kwa niaba ya uongozi wa hoteli na kumkaribisha kwa mara nyingine tena.Denis aliingia ndani ya gari lake na kuelekea Kisosora kumchukua Bi Zena.
Alipofika alipokelewa na Mzee Kambi na kumwambia kuwa mkewe yupo chumbani anajiandaa.Waliendelea na maongezi pale barazani huku muda ukizidi kuyoyoma bila Bi Zena kutokea.Denis alishangazwa sana na hali ile mpaka akadhani pengine mama huyo ameghairi safari.
“Mzee mbona mkeo hatoki kuna tatizo gani?”Baada ya uvumilivu kumshinda,Denis aliamua kuuliza kulikoni.
“Wewe mama Shaimaa.”Mzee Kambi aliita kwa sauti ya juu.
“Abee mume wangu.”
“Unafanya nini huko ndani mwaka mzima?Muda haukusubiri wewe,unamchelewesha kijana wa watu hapa.”
“Nakuja.”
“Haya fanya haraka.Usijali kijana,anakuja sasa hivi.”Dakika ishirini zilipita tena bila Bi Zena kutokea.
“Mzee vipi,mbona hatoki tena?”Denis alihoji kwa hasira.
“We mama Shaimaa!”
“Ndiyo nakuja jamani.Hee!kwahiyo nisijitengeneze?Mwanamke urembo babu wewe!”
“Haya mimi sikuwezi.”Mzee Kambi aliongea kinyonge.
Mama huyo alipotoka nje hakutamanika.Jini siyo jini,msukule siyo msukule.Yaani kifupi ni kwamba hakueleweka kama ni msichana au mama mtu mzima.Alikuwa amejipara si mchezo.Alipaka rangi za aina tofauti tofauti katika macho yake.Mdomo aliukoleza kwa rangi nyekundu huku uso wake akiumiminia poda kopo zima.Vile vile alijimwagia urembo mwingine uliokuwa unametameta na kuufanya uso wake kuonekana kama ukumbi wa disko.
Kichwani alijivika manywele ya bandia yaliyozidi kuupoteza uhalisia wake.Pia alikuwa amejichora kwa ina mwili mzima.Muonekano wake ulimkera sana Denis lakini alishindwa kumwambia ukweli mama huyo.Aliishia kumwangalia kwa hasira huku akimezea maneno yake ndani kwa ndani ili asionekane mtu aliyekosa heshima mbele ya watu wazima.
“Shoga,naona umeshatokelezea,wapi hiyo?”Wakati mama huyo akiwa anapeleka begi lake kwenye gari mara mashosti zake wawili wakatokea kufuata ubuyu.
“Naelekea zangu Dar kula maisha.”Bi Zena alijibu kwa mbwembwe.
“Unaenda Dar mwenzetu!”
“Sasa je!”
“Kwa nani?”
“Si mnamuona huyo dogodogo wangu hapo?”
“Namuona,halafu inaelekea mambo safi si mchezo.”
“Mmmh!shoga,huyo ni bonge moja la tajiri.Kama nisipompata mimi basi lazima mwanangu Shaimaa amnase.”Bi Zena alijitamba.
“Loo!inamaana bado hujamuonjesha tu?”
“Bado shoga,ndiyo kwanza nimeanza naye mazoea juzi juzi tu.Sasa hivi tunamuhamishia Shaimaa Muhimbili na huyu ndiyo analipa kila kitu.”
“Basi nikuambie kitu shosti?”
“Nipe ubuyu huo.”
“Huyu muache Shaimaa ndiyo atamnasa vizuri.”
“Sawa,lakini siku hizi mwanangu anajifanya kaacha mambo hayo eti yupo bize anawatunza watoto wake kwa kuuza Uono.”

“Shoga,itabidi tumkalishe chini tumwambie.Hii ni bahati na siku zote huwa haiji mara mbili.Yeye ashangae shange ataishia kuuza Uono wenzake wanatembelea magari.”
             *******
Je nini kitaendelea?Usikose sehemu ijayo ya simulizi yetu iliyojaa visa na mikasa ya kusisimua.Naamini unaendelea kujifunza siku hadi siku na pia unaburudika vya kutosha.Nakutakia siku njema na Mungu akubariki sana.
             *******
Kwa maoni au ushauri napatikana kwa namba 0655089197/0766123623

Share this

Related Posts

Previous
Next Post »