STORY-PENZI LA MSHUMAA
MTUNZI-MZIRAY F.M
SEHEMU YA 12
Ilipoishia sehemu ya 11
“Ungekuwa hujamgonga wewe ungenipa fedha ili tuyamalize?Kwanini unataka kumkimbia binti wa watu wakati wewe ndiyo umemvunja miguu?Tumeshakumbana sana na kesi nyingi za namna hii ndiyo maana sasa hivi hatutaki mchezo hata kidogo.Kuna watu wamekaa humu hospitali huu ni mwaka wa pili kwa kukosa msaada baada ya kukimbiwa na ndugu zao au watu kama ninyi mliowasababbishia matatizo.Sasa hivi tumekuwa macho hatutaki suala hili lijirudie tena.”

Sasa endelea.......
Yule dokta alizungumza kwa hisia kali akilalamikia vitendo vya watu kuwasusia wagonjwa wao pale hospitali bila msaada wowote.Aliamini kuwa Denis ni mmoja wa watu kama hao baada ya yule binti kukiri kuwa Denis ndiyo kamsababishia ajali.
“Ila dokta mnanione tu,mimi sihusiki na ajali hiyo.”Denis alizidi kujitetea.
“Hayo masuala utakuja kuwaleza polisi watakapofika hapa.”Dokta hakutaka malumbano na Denis badala yake alimwambia kuwa awasubiri polisi wafike ndipo ajitetee.Denis hakuwa na jinsi,aliamua kudondosha shingo yake chini kwa masikitiko.Baada ya dakika tano polisi wakiwa na silaha mkononi walifika pale hospitali na kueleza kuwa walipigiwa simu na mmoja wa madaktari wa pale.Wakati Denis akiwa kajiinamia chini mara simu ya yule dokta aliyekuwa naye ikaita.
“Hello!habari ni nzuri tu.”dokta alipokea simu na kuanza kuongea. “Yaa!mimi ndiyo niliwapigia,waelekeze katika chumba changu.Haya okay,nashukuru sana.”Denis aliinua uso wake na kumtazama yule dokta kwa hasira.Kabla hajafanya kitu chochote mara mlango wa kile chumba ukagongwa mara mbili.
“Ngo!ngo!”
“Pita tu mlango upo wazi.”Dokta alitoa ruhusa ya aliyekuwa anagonga kuingia ndani ya chumba.


“Oooh!maafande karibuni sana.Kijana mwenyewe anayeleta mushkeli kidogo ndiyo huyu hapa.Amesababisha ajali halafu anataka kukimbia.Amemgonga binti mmoja ambaye kwa sasa yupo hodini na kumvunja miguu yote.Sasa anataka kumtelekeza halafu yeye ayoyome zake.Mambo haya yameshatokea sana hapa hospitali na ndiyo maana safari hii tukawa makini mno.”Dokta aliwaeleza wale askari sababu iliyomfanya awaite pale
“Dokta nimeshakwambia huyo binti ni muongo.”
“Funga mdomo wako.Pumbavu!”Askari mmoja alimnyamazisha Denis kwa sauti ya ukali.
“Nyie ndiyo mnaua watu halafu mnawakimbia siyo?Dokta,tunaweza kuzungumza na huyo binti ili athibitishe hili suala?”Askari mwingine alidakia na kumuuliza dokta kama kuna uwezekano wa kumsikia binti mwenyewe akizungumza.
“Hakuna tatizo tunaweza kwenda kumuona.”Dokta aliwachukua wale askari wakiwa na Denis kuelekea katika kile chumba alicholazwa yule binti.Baada ya kufika askari mmoja alianza kumhoji taratibu.
“Binti unaitwa nani?”
“Naitwa Shaimaa.”Yule msichana alijibu kwa sauti ya chini.
“Pole sana binti kwa yaliyokukuta.”
“Asante afande.”
“Unamfahamu huyu kijana?”Denis alisogezwa karibu na yule binti aliyejitambulisha kwa jina la Shaimaa.
“Ndiyo namfahamu.”
“Tumepigiwa simu na kuambiwa kuwa anataka kutoroka.Sasa tumekuja hapa ili kupata maelezo yako juu ya ajali iliyotokea.”Maelezo aliyoyatoa Shaimaa hayakutofautiniana na yale maelezo aliyowapa wale madaktari mwanzoni.Alizidi kushikilia msimamo wake kwamba Denis ndiyo aliyemgonga kwa gari lake la kifahari.Kauli hiyo aliitoa huku akiwa anamwaga machozi kwa kumlaumu kijana huyo kuwa amempa ulemavu wa maisha.
“Huyu binti katumwa nini?We dada,una uhakika kuwa mimi ndiyo nimekugonga?Muulizeni aliniona vipi wakati yeye alikuwa kwenye pikipiki.”Denis alishindwa kuelewa ni jinamizi gani limekumba ndani ya jiji hilo.
“Kelele wewe.”Afande mmoja alimfokea Denis.
“Siyo suala la kelele.Dokta,hebu mpimeni huyo msichana pengine amechanganyikiwa.”
“Mimi sijachanganyikiwa wala nini.Wewe ndiyo umenigonga kwa gari lako.Nilikushuhudia kabisa kwa macho yangu ukiniletea gari miguuni wakati nilipokuwa navuka barabara.Watu walikusihi upunguze mwendo lakini hukutaka kusikia.Baada ya kunigonga ukajidai eti unanisaidia kinafki ili raia wenye hasira kali wasikushambulie.Umefika hapa unataka kunikimbia ilihali umeshaniharibia maisha yangu.”Shaimaa aliendelea kukazia maelezo yake.
“Haaa!hata aibu huna!Mungu wangu!wema wangu ndiyo umeniponza.Kwahiyo bora ningekuacha pale pale ufe kuliko huu usamaria nilioufanya?”Moyo wa Denis ulikunjwa ndita kwa hasira.Alitamani amrukie Shaimaa pale alipolala na kummaliza lakini aliona atajizidishia matatizo zaidi.Sekunde kadhaa baada ya Denis kumaliza kuongea mara mlango wa chumba kile  ukafunguliwa akaingia nesi akiwa na watu wanne.Kulikuwa na baba mmoja wa makamo kidogo na mama mmoja aliyeeonekana kama mkewe.Vile vile walikuwa na mabinti wawili waliokwishavunja ungo.
“Oooh!mwanangu Shaimaa pole sana kwa yaliyokukuta.Uuuwiii!mwanangu umeshakuwa kilema.Eeeh Mungu kwanini umeiandama familia yetu kiasi hiki?”Yule mama alianza kupiga mayowe baada tu ya kumwona Shaimaa akiwa kalala juu ya kitanda cha wagonjwa.
“Mamaaa!mamaaaaa!mwanao nakufa!Baba!baba mtoto wako nimeshakuwa mlemavu!Nitaishije mimi jamani mie.”Shaimaa naye alipowaona wazazi wake alianza kupiga kelele za uchungu.
Daktari pamoja na nesi waliwasihi wapunguze kelele kwani mgonjwa anaweza akazidiwa kutokana na uchungu atakaoupata.Mama alimfuta mwanaye machozi na kumbusu kwenye paji la uso wake.Baba alisalimiana na watu wote waliokuwa ndani ya chumba kile.Pia mama alifanya kama mume wake alivyofanya na wale wasichana nao wakafuata.
Wakati Denis alipokuwa kwa daktari,Shaimaa alimpatia nesi namba za wazazi wake na kuwasiliana nao ili kuwaeleza hali iliyompata binti yao.Baada ya nesi kuwapigia wazee hao na kuwapa habari hizo,walifunga safari wakiwa roho juu juu mpaka Bombo hospitali ambapo walielekezwa chumba alicholazwa Shaimaa na kwenda kumtazama.
“Kwahiyo maafisa mmefanikiwa kumkamata huyo kijana aliyemgonga binti yangu?”Maelezo aliyoyatoa yule nesi wakati alipowasiliana na wazazi wa Shaimaa ndiyo yale yale aliyowaleleza binti huyo kuwa aligongwa na gari wala siyo pikipiki.Jambo hilo lilimfanya Mzee Kambi ambaye ni baba yake Shaimaa kuwahoji wale polisi waliokuwepo ndani ya hodi ile.
“Usiwe na wasiwasi mzee,kijana mwenyewe tunaye hapa.”Askari mmoja alijibu kwa kujiamini.
“Yupo wapi?Au ndiyo huyu hapa?”Mzee Kambi aligeuka na kumtazama Denis aliyekuwa ameshikilia funguo za gari lake huku nguo zake zikiwa zimetapakaa damu.
“Haswaaa,ndiyo huyu.”Askari mmoja alimthibitishia mzee huyo kuwa aliyekuwa anamtazama ndiyo kijana aliyemgonga binti yake.
“Kijana unataka kuniulia mwanangu,shenzi kabisa!Zaa wako umtoe roho.”Mze Kambi aliinuka na kutaka kumvamia Denis kama tingatinga lakini askari waliweza kumdhibiti asifanye kitendo hicho.Alitulizwa na kuambiwa kuwa asiwe na shaka kila kitu kitakuwa sawa kabisa kwasababu mtuhumiwa yupo mikononi mwao.Japokuwa mzee huyo alionekana mwenye afya mgogoro lakini ni mshari balaa!
“Usipaniki mzee,huyu kijana tayari yupo katika mikono ya chombo cha dola hivyo acha sheria ichukue mkondo wake.”Denis alimkata Shaimaa jicho la hasira kutokana na kumsingizia kosa ambalo hakulitenda yeye.
“Unamwangalia nini mwanangu?Ulitaka kumuua halafu sasa hivi unamwangalia kwa macho yako ya kichawi!Mwanga mkubwa wewe.”Mama yake Shaimaa anayejulikana kwa jina la Bi Zena alikasirishwa mno na kitendo cha Denis kumwangalia binti yake.Hapakuwa na jinsi,Denis alifungwa pingu na kutolewa nje ya jengo lile.
Waliingia ndani ya gari lake ambapo askari mmoja aliendesha mpaka kituoni maeneo ya Raskazoni.Walipofika kituoni Denis aliingizwa chumba cha mahojiano na kuanza kuhojiwa. “Kijana kwanini umegonga mtu halafu unataka kukimbia?”
“Afande naongea ukweli kabisa mimi sijamgonga yule binti.Alipata ajali ya pikipiki pale kwa Kwaminchi karibu na reli.”Denis alijaribu kujitetea.
“Nyamaza!unadhani sisi ni watoto wadogo au?Huu ndio mchezo wenu wa kila siku.Mkishakuwa na magari ya mikopo basi mnajiona ndiyo mmefika mnatawala barabara nzima.Hivi kwanza una leseni kweli wewe?”
“Ndiyo,ninayo.”Denis alijibu kinyonge.
“Ipo wapi?”
“Kwenye gari.”

“Twende ukaichukue.”Denis alitolewa nje akiwa na pingu zake mkononi.Walielekea moja kwa moja mpaka kwenye gari na kutoa leseni katika begi lake.
             ********
Itaendelea....Nashukuru kwa ufuatiliaji wako wa hadithi hii...Nakutakia siku njema na Mungu akubariki sana.
            *********
Kwa maoni au ushauri napatikana kwa namba 0655089197/0766123623

Share this

Related Posts

Previous
Next Post »