STORY-PENZI LA MSHUMAA
MTUNZI-MZIRAY F.M.
SEHEMU YA 18
Ilipoishia sehemu ya 17
“Tena mtihani mzito kweli kweli kwa wazazi wa huyu binti siyo kwako.Umewatia dosari ya maisha.Wameniambia kuwa huyo binti ndiyo tegemeo lao pale nyumbani.Wao hawana shughuli yoyote ya kuwaingizia kipato.Wamesema kuwa Shaimaa ndiyo alikuwa anatoka na kwenda kubangaizabangaiza mitaani na kuwaletea chochote kitu.Tangu mtoto wao apate ajali hawajaingiza chochote mdomoni na ukizingatia wanaishi na mabinti wadogo wawili wanaosoma.Wamekilaumu sana kitendo ulichomfanyia binti yao ambacho kimeathiri familia nzima.Kwahiyo kijana tambua kuwa laana ya wazee hao itakusumbua maisha yako yote.”

Sasa tiririka nayo......
Dokta alimweleza Denis mambo ambayo yaliuumiza sana moyo wake.Japokuwa yeye hakuhusika kwa chochote kile juu ya ajali ya Shaimaa lakini hali ya familia yake ilimpa sononeko la moyo.Kitendo cha kusikia kuwa Shaimaa ndiyo alikuwa mhimili wa familia yao kilimsikitisha sana.
Shaimaa alikuwa anafanya biashara ya kuuza dagaa wabichi wanaojulikana kwa jina maarufu la Uono huko mkoani Tanga.Mtaji wake ulikuwa ni mdogo sana hivyo hakuwa na biashara kubwa ya kuridhusha.
Alikuwa anapitisha nyumba hadi nyumba kwa kutumia baiskeli yake aliyoifunga kikapu cha dagaa kwa nyuma.Faida iliyopatikana ilikuwa ni kidogo mno ambayo ilitumika kununulia mlo wa siku.
Wazazi wake hawakuwa na kazi yoyote ile ya kuwaingiza kipato.Baba yake Shaimaa,Mzee Kambi muda wote alishinda kwenye vilabu vya pombe ya mnazi.Vile vile alikuwa ni maarufu sana kwa mchezo wa bao ambapo aliwanyanyasa wazee wenzake kila kukicha.Wakati mwingine alipokosa pesa ya kununulia pombe aliingia chumbani kwa binti yake na kumwibia fedha zake za biashara.Akitoka asubuhi anarejea saa 6 usiku ambapo analeta vurugu nyumba nzima.
Mke wa mzee huyo,Bi Zena,naye alikuwa hajatulia hata kidogo.Muda wote alijipamba kwa kujichora ina mwili mzima sambamba na kutinda nyusi zake na kutengeneza kope.Akishapendeza anaelekea kwa mashangingi wenzake ambapo walipiga domo kuanzia asubuhi hadi jioni.Wakishatoka hapo wanatafuta sehemu yenye kigodoro na kwenda kukata mauno mpaka asubuhi.Naye suala la kulewa ilikuwa ni kawaida yake tena kushinda hata mumewe.
Pombe hizo alikuwa ananunuliwa na vijana wadogo ambao ni sawa na watoto wake na mwisho wa siku wanaenda kulipana gesti.Mwanzoni Shaimaa naye alikuwa na tabia kama ya mama yake lakini baada ya kudungwa mimba mara mbili akapata akili.Aliamua kupambana kwaajili ya wanaye baada ya kususiwa na baba zao.Alijaribu kila njia kuwashauri wazazi wake ili waachane na tabia hizo lakini jitihada zake zote ziligonga mwamba.
Wazee hao hawakuwa na sehemu nyingine yoyote ya kupata chakula zaidi ya pale nyumbani.Hivyo basi,Shaimaa ndiyo alikuwa tegemeo lao kwa kila kitu.Hawakubahatika kupata mtoto mwingine zaidi ya binti huyo katika maisha yao ya ndoa.
Ilifikia hatua wazee hao wakawa na madeni kila kona baada ya kukopa pesa za pombe.Binti huyo ndiye aliyekuwa na jukumu la kupunguza madeni hayo siku ambazo biashara zake zilikwenda vizuri.Kwasababu binti huyo alikuwa maarufu sana pale mtaani kwao kutokana na tabia ya familia yake,ilimuwiya vigumu mno kuanzisha biashara hiyo ya dagaa aina ya Uono kwa mara ya kwanza.Vijana wenzake hasa wasichana walimcheka sana mpaka akatamani kuiacha.
Lakini kila alipowatazama watoto wake aliwaonea huruma hivyo ikamlazimu kupambana.Hakuona umuhimu tena wa kuugawa mwili wake ovyo kwa wanaume ili wamapatie msaada kama alivyokuwa anafanya kipindi cha nyuma akiwa na marafiki zake.Kila siku alfajiri Shaimaa alidamka na kuelekea baharini kununua hao dagaa wabichi toka kwa wavuvi na kuanza kuwapitisha mitaani.
Biashara hiyo ndiyo iliyowawezesha wanafamilia hao kuingiza mkono kinywani na kuelekea msalani.Hivyo basi,tangu Shaimaa alipopata ajali hali imekuwa siyo hali pale nyumbani.Hata kupata mlo wa siku imekuwa ni tabu.Si baba wala mama aliyekuwa na kazi ya kufanya.Walikuwa na madeni kila mtaa ndiyo maana walishindwa hata kwenda kukopa unga angalau wapike hata uji wa tangawizi.Hali hiyo ndiyo iliyowafanya wazee hao wamlaani Denis wakiamini kuwa yeye ndiyo aliyeleta matatizo katika familia yao baada ya tegemeo lao kuishia kulala tu kitandani bila matumaini yoyote.
Denis aliinamisha kichwa chake chini na kushusha pumzi ndefu baada ya daktari kumweleza hali halisi ya Shaimaa ilivyokuwa mbaya pamoja na hali ya wazazi wake.Aliinua tena uso wake na kumtazama dokta usoni kisha akamtwanga swali.
“Naweza kumwona mgonjwa?”
“Hapana,kwa sasa hivi yupo katika chuba maalumu cha upasuaji ambapo madaktari walikuwa wanashughulika naye bila matumaini.”Dokta alimweleza Denis kuwa hatoweza kumuona Shaimaa kwa wakati ule.
“Kwahiyo gharama za matibabu mpaka sasa hivi ni kiasi gani?”Denis alipigiwa mahesabu ya gharama zote alizotumia Shaimaa katika matibabu na baada ya kupewa alitoa pochi yake na kuzilipa pesa zote.Alipewa risiti yake kisha akataka kujua utaratibu wa kumwamishia mgonjwa Muhimbili.
“Sisi tutakuandikia hapa,tutakupa kadi pamoja na faili lake kisha utakwenda pale Muhimbili kwenye kitengo cha mifupa.Ukishafika hapo madaktari watamwangalia mgonjwa na huduma itaanza mara moja.”
“Kwahiyo kuna uwezekano wa kuondoka naye lini?”
“Nafikiri keshokutwa kwasababu leo ndiyo kapata huo upasuaji mwingine mdogo.Nadhani siku ya kesho ataitumia kwa mapumziko halafu hiyo keshokutwa muondoke naye.”
“Nashukuru sana dokta,ngoja nikajaribu kuzungumza na wazazi wa binti huyo maana wamenishupalia mno.”
“Usijali,ngoja tuende wote nikawaeleweshe.”
“Nitashukuru sana.”Dokta na Denis walitoka nje ya chumba kile kwa lengo la kwenda kuzungumza na wazazi wa Shaimaa waliokuwa wamefura kwa hasira.Moyo wa Denis ulishafunguka na kukubali kuubeba mzigo usiomhusu.Maelezo ya yule dokta kuhusu hali ya familia ya binti huyo jinsi ilivyo iliuchoma moyo wake na kuamua kutoa msaada kwa roho nyeupe kabisa.
“Dokta vipi hali ya binti yetu?”Walipofika nje,Bi Zena aliinuka kwa shauku ya kutaka kujua hali ya mwanaye.
“Hali ya mtoto wenu siyo nzuri sana lakini kuna tumaini la………….”
“We nyang’au unaona sasa ulivyoingiza balaa katika familia yetu?Umeshamuua mtoto wetu na hatujui tutaishije tena pale nyumbani.Yeye ndiyo kila kitu kwetu.Kama akifa nakuhakikishia hata wewe hutochukua raundi lazima umfuate.”Mzee Kambi hakutaka hata kusikiliza maelezo ya daktari.Alimrukia Denis kwa maneno na vitisho vya hali ya juu.
“Sikiliza kwanza mzee wangu,hebu punguzeni munkari ili tuelewane.”Dokta alijaribu kumpoza Mzee Kambi.
“Apunguze munkari wa nini?Au kwa kuwa siyo mtoto wako aliyepata matatizo?Nakuambia hivi kijana,mwanangu akifa lazima umtafune nyama.Shaimaa ndiyo alikuwa tegemezi letu halafu wewe kwa makusudi ukaamua kumvunja miguu yake.Sijui umetumwa we mwanga!”Bi Zena naye hakutaka kutulia.Alifunga kibwebwe kwaajili ya kumpasha Denis.Nyoyo zao zilijaa jazba ya hali ya juu  kutokana na majanga aliyoyapata binti yao ambapo waliamini kuwa Denis ndiyo chanzo cha yote hayo.
“Nadhani kila mmoja akiwa na jazba hatutaweza kutatua jambo lolote hapa.Chamsingi ni kuzipunguza hasira zetu ili tujue tunaokoaje maisha ya Shaimaa.”Baada ya wazee wale kupiga sana kelele mwishowe wakachoka na kuamua kutulia.Denis aliumia sana moyoni kwa kupewa shutuma zisizomhusu.Kuna wakati aliwaza kusitisha kabisa msaada wake na kulipeleka shauri hilo mahakamani ambapo aliamini kuwa huko haki ingetendeka.
Lakini alipokumbuka maelezo ya dokta kuwa Shaimaa ndiyo alikuwa mhimili wa familia yao moyo ukamsuta.Aliamua kujikaza kiume ili amuokoe binadamu mwenzake.Hakutaka kuutumia utajiri wake vibaya badala yake alipenda kuwasaidia wasiokuwa nacho lakini si kwa kusingiziwa kosa ambalo siyo lake.
“Nimezungumza na kijana hapa amekubali kulipa fedha za kumhamishia binti yenu Muhimbili jijini Dar-es-salaama akapate matibabu ya kina zaidi.Msiwe na wasiwasi Shaimaa lazima apone.”Dokta aliwaleza hayo wazazi wa Shaimaa kwa sauti ya upole.
“Sina hakika kama mwanangu atapona.Si ulisema anaweza akakatwa miguu yake?”Bi Zena alizungumza kwa unyonge.Hakuwa na imani kama mwanaye atapona tena na kurudi katika hali yake ya kawaida.
“Kwa kuwa anakwenda Dar-es-salaam kwenye hospitali ya taifa hakuna shaka kabisa lazima atakuwa vizuri.La muhimu ni kumwomba Mwenyezi Mungu atie baraka zake na kila kitu kitakuwa salama salimini.”
“Sawa dokta tumekuelewa lakini tambua kuwa Shaimaa ndiyo alikuwa tegemeo letu pale nyumbani.Sasa hivi hatuna msaada wowote ule.Kama tulivyokuambia leo ni siku ya tatu hatujala chochote zadi ya  kunywa tu maji.”Bi Zena alianza kueleza matatizo ya familia yake kwa uchungu.
“Hilo halina tatizo mama.Mimi nitabeba jukumu la kuwahudumia mpaka pale mtoto wenu atakapopona.Kwahiyo kwa hilo wala msijali kabisa,tupo pamoja.”Na maneno yote ya kejeli na lawama alizopewa lakini Denis bado alikuwa na moyo wa kuwasaidia wanafamilia wale.
“Mmmmh!kwa jinsi navyokuona na roho mbaya yako utatusaidia kweli?”Mzee Kambi bado alijifanya jeuri.Msaada aliuhitaji lakini hakuacha kuendelea kutoa lawama zake kwa Denis.Uchungu uliendelea kuutafuta moyo wa Denis lakini alijikaza kiume.Denis aliwachukua wazee hao na kuwapeleka Dophin hoteli na kuwanunuliwa kufungua kinywa cha nguvu.Mzee Kambi na mkewe hawakuamini kilichotokea.

Tangu wazaliwe hawajawahi kuingia katika hoteli ya kisasa kama hiyo na kupata msosi wa namna ya kipekee.Muda wote walikuwa wanashangaashangaa kama vile wapo feri.Baada ya kumaliza kupata kifungua kinywa Denis aliwaingiza wazee wale ndani ya gari lake na kuanza safari ya kuelekea nyumbani kwao katika kata ya Chumbageni maeneo ya Kisosora.Walipita kwenye mzunguko wa pale Kwaminchi na kunyoosha barabara ambapo baada ya kuuvuka msikiti walikata kushoto na kuendelea na safari.
                 ********
Je nini kitafuata?Usikose mwendelezo wa simulizi hii iliyojaa visa na mikasa ya kusisismua siku ya Jumatano.Natumaini unaburudika na unaendelea kujifunza mengi kila iitwapo leo.Nakutakia siku njema na Mungu akubariki sana.
               ******
Kwa maoni au ushauri napatikana kwa namba 06550891987/0766123623

Share this

Related Posts

Previous
Next Post »