STORY-PENZI LA MSHUMAA
MTUNZI-MZIRAY F.M.
SEHEMU YA 17
Ilipoishia sehemu ya 16
Baada ya mawazo hayo kuanza kupotea ndani ya kichwa cha Denis,taratibu usingizi ukaanza kumnyamelea mdogo mdogo.Hakujua hata amelala saa ngapi lakini alikuja kushtuka baada ya kudondokewa na matone ya maji baridi usoni.Alipofungua macho yake alimuona Vivian akiwa na glasi ya maji mkononi.

Sasa endelea....
“Denis amka acha uvivu.Unajua sasa hivi ni saa ngapi?”Vivian alimwambia hayo Denis baada ya kumwangalia kwa macho yaliyokabwa na usingizi.
“Kwani saa ngapi?”Denis aliuliza kivivu.
“Saa mbili.”
“Saa mbili!Mbona umeshapendeza saa hizi,unakwenda wapi?”Denis alimshangaa mchumba wake aliyekuwa anawaka ndani ya mavazi yake ya heshima.
“Ndiyo tunaondoka hivyo.Akina Brenda wamenipigia simu na kuniambia kuwa wameshajiandaa kwa safari.”
“Duuuh!mbona hawajanishtua?”
“Wamekupigia simu zaidi ya mara nne sema tu tulikuwa tumelala na simu yako sijui umeiweka wapi?Kuona hupokei ndiyo wakaamua kunipigia mimi.”Denis alipopata taarifa hizo alikurupuka toka kitandani na kujifunga taulo.
“Simu yangu sijui nimeiweka wapi?Hebu piga namba yangu nisikie inapoitia.”Vivian alichukua simu yake na kumpigia Denis. “Inaita?”Denis aliuliza
“Ndiyo.”
“Inaitia wapia sasa mbona siisikii?”
“Nasikia mlio kwa mbali sijui ni wapi.Hebu angalia kwenye suruali yako.”Denis alipokwenda kucheki ndani ya suruali yake alikuta simu iliyokuwa na missed calls tano.Mbili za Dick,moja ya Brenda,nyingine ndiyo hiyo ya Vivian aliyepiga muda huo huo walipokuwa wanaitafuta simu hiyo.Moja ilikuwa ni namba ngeni kabisa katika simu ya Denis.Aliachana nayo akaingia bafuni kusafisha mwili wake.
Alipotoka alivaa nguo zake kisha akafuatana na Vivian mpaka nje ya hoteli.Alipiga namba ya Dick ikawa inatumika akaamua kumpigia Dolan.Alimwambia kuwa Vivian yupo tayari kwa safari hivyo wampitie pale hotelini.Baada ya dakika tano akina Brenda waliwasili pale Dolphin hoteli.Brenda akiwa na wenzake walimkumbatia Denis na Vivian kwa furaha ya ajabu.
“We Denis ulikuwa umelala usingizi wa pono nini?Mbona tumekupigia simu mara kibao hujapokea?”Dick alianza kumshambulia Denis kwa maswali.
“Ha!ha!ha!ha!ha!nisameheni jamani nilikuwa nimesahau simu kwenye suruali yangu.”Denis alijitetea.
“Umesahau simu wapi sema mahaba yalikubana.”
“Ha!ha!ha!ha!ha!ha!”
“Waooooh!Dolan hapo umeongea.Maana Vivian akimkamata Denis kwenye kona yake huwa hatoki kaka yangu huyu.”Winfrida aliunga mkono kauli ya Dolan na wote wakacheka kwa pamoja.Vivian alimkumbatia Denis na kuuficha uso wake kwa aibu.
“Ha!ha!ha!ha!Vivian twende,sisi ndiyo tunaondoka hiyo.Au umeshapata wazo la kubaki Tanga ghafla?”Brenda alitaniana na wifi yake ambapo furaha iliendelea kutawala eneo lile.
“Huyu mwacheni nampakia kwenye gari yangu mpya nawasindikiza mpaka Kange stendi kuu.Tukishafika hapo ndiyo atakuja kupanda hicho kibatari chenu.”Denis alimng’ang’ania mchumba wake na kuwaringishia ndugu zake.
“We jishaue tu na Range Rover lako.Tungejua tusingekuja kukutoa,ungeozea mahabusu.”Brenda naye aliingiza utani wake na kufufua vicheko kwa wenzake.
“Ha!ha!ha!ha!ha!ha!hilo nalo neno.”
“Ha!ha!ha!ha!uliona jinsi Vivian alivyochimbwa mkwara na yule afande?”Dick alitoa la kwake.
“Ha!ha!ha!ha!alikuwa anatetemekaje!Na ukome kuropokaropoka ovyo.Kama siyo huyu mumeo kujitoa muhanga ungekuta na wewe upo ndani.”Brenda alizidi kupigilia msumari.Baada ya utani wa hapa na pale waliingia kwenye gari na kuanza safari ya kurudi Dar-es-salaam.Walipofika maeneo ya Kange stendi mpya Denis alimshusha Vivian ambapo alienda kuingia kwenye gari walilokuja nalo Tanga.
“Mhudumie vizuri mgonjwa wako feki.”Winfrida alichungulia dirishani na kumrushia dongo kaka yake.
“Nendeni zenu huko.Kwaherini jamani nawatakia safari njema.Bye!bye!msijali wiki ijayo nitakuja huko.”Denis aliagana na ndugu zake haoo wakayoyoma zao.Baada ya hapo Denis aligeuza gari na kuanza kurejea hotelini mdogo mdogo.Wakati akiwa kwyene gari Denis alitoa simu yake akawa anapitiapitia mambo fulani yanayohusu biashara zake.Mara akakumbuka kuwa kulikuwa na namba mpya iliyompigia asubuhi lakini hakuipokea.Aliitafuta hiyo namba kwenye orodha ya simu zilizoingia na kuikuta.Alibonyeza kitufe cha kupigia na kuiweka sikioni.Iliita kidogo tu mara ikapokelewa.
“Hello!habari yako kijana?”Upande wa pili ulimjulia hali Denis baada ya kupokea simu.
“Habari ni nzuri tu,shikamoo.”Denis alisalimia na kutulia.
“Marahaba.Sasa ni hivi,mimi ni Mzee Kambi baba yake Shaimaa.”Upande wa pili ulijitambulisha.
“Baba yake Shaimaa,mmh!Shaimaa!Bado sijakupata vizuri,Shaimaa wa wapi?”Denis alitaka ufafanuzi zaidi.
“Nipo Bombo hospitali.Ni baba wa huyu binti uliyempa ulemavu.”Mzee alizungumza kwa ukali kidogo baada ya kuona kuwa Denis hamwelewi.
“Ooooh!nimeshakupata vizuri.Samahani sana mzee wangu,hilo jina la Shaimaa kidogo bado sijalishika ndiyo maana ikawa shida kukufahamu kwa haraka.Ehe!vipi hali ya mgonjwa?”
Japokuwa Denis aliumia baada ya Mzee Kambi kuendelea kumshutumu kuwa yeye ndiye aliyemgonga binti yake,lakini alijikaza kiume na kuzungumza naye kistaarabu.
“Kwa kweli hali siyo nzuri hata kidogo.Tunakuomba hapa hospitali mara moja.”
“Kwani kuna tatizo gani mzee?”
“Tatizo lipo tena kubwa sana kuhusu binti yangu.”
“Haaa!kuna usalama kweli hapo?”
“We njoo kila kitu utakuja kukijulia huku huku.”
“Haya nakuja sasa hivi.”Denis alishtuka sana baada ya kuambiwa kuwa hali siyo nzuri kule hospitali.Alikanyaga mafuta na kuongeza mwendo kuelekea mjini.Kabla hajaikamata barabara ya Raskazoni,Denis alipaki gari pembeni na kuanza kutafakari. “Hivi kuna usalama kweli huko ninapokwenda?Isijekuwa najitumbukiza mwenyewe kwenye mdomo wa Simba!Sijui niende,sijui nisiende?Daah!hii mbona kazi.Nilishajihukumu mimi mwenyewe acha tu niende.”
Denis aliingiza gari barabarani na kuongeza mwendo kuelekea Bombo hospitali.Japokuwa hakuwa na uhakika wa huko aendako lakini ilimlazimu kwenda hivyo hivyo kichwa kichwa tu.Alipofika hospitali alipokelewa na huzuni iliyokuwa imewatawala wazazi wa Shaimaa.
“Shikamooni wazee wangu.”Denis alisalimia kwa heshima.
“Unamsalimia nani?Kama hizo shikamoo zingekuwa mali ungekuta sasa hivi tunamiliki ghorofa.”Mzee Kambi alimkaripia Denis kwa hasira.
“Aaaah!jamani,mimi si ninawasalimia tu!Kwani kuna tatizo gani?”Denis alipigwa na butwaa.
“Hebu tupishe huko mnafki mkubwa wewe.Wewe si ndiyo umemsababishia mwanetu hayo matatizo.Na kama akifa lazima umle nyama labda mimi siyo Bi Zena.”Mama yake Shaimaa naye alilipuka kama petrol.
“Bado sijakuelewa mama,unamaanisha nini kusema hivyo?”
“Bado hujanielewa eeeh!Utatuelewa tu baada ya tegemeo letu kufa.”Denis alibaki njia panda asijue wale wazee wanamaana gani kusema vile.Moyoni aliumia sana kwa kuendelea kushutumiwa kwa kosa lisilomhusu.Nani anaweza kusimama na kumtetea?Ukweli wote alikuwa nao Shaimaa ambaye ndiyo anaweza kubadilisha mawazo ya watu juu yake.Lakini ndiyo hivyo,msichana huyo bado aliendelea kushikilia msimamo wake kuwa Denis ndiye kahusika na ajali yake.Aliwatazama wale wazee walivyokuwa wanamshumbulia kwa maneno ya lawama hadi akajikuta amedondosha chozi la uchungu.
“Unajifanya kulia!Unalia kitu gani?Unajiliza unafki tu hapa.Kisa umeona una fedha basi ukaamua kuiharibu nguzo yetu ya familia.Kwahiyo sasa hivi roho yako nyeupee,furaha imekutawala.Azma yako ya kutumia pesa zako vibaya kwa kuwanyanyasa wasiokuwa nacho imeshatimia sasa.Usijifnye kumlilia mwanangu wakati wewe ndiyo umemwingiza katika matatizo haya kwa makusudi.”Mzee Kambi aliendelea kumzonga Denis huku akiwa kaukunja uso wake kwa hasira.Hata hivyo Denis hakujibu chochote,aliamua kuingia chumba cha daktari ili akaulizie hali ya Shaimaa.
“Haa!kijana umerudi tena?karibu sana.”Denis alipoingia kwa daktari alikumbana na yule dokta aliyemuitia polisi wakaja kumkamata.Alitamani arudi lakini alipoikumbuka hali aliyoiacha nje ikamlazimu kuzungumza tu na yule daktari.
“Habari siyo nzuri dokta,nataka nifahamu maendeleo ya Shaimaa.”Denis aliuliza akiwa wa motomoto.
“Kwanza umekutana na wazazi wa huyo binti?”Dokta aliuliza.
“Ndiyo.”
“Umeona hali zao?”
“Dokta niambie huyo binti anaendeleaje.Habari za wazee wake za nini sasa hapa?”Denis alikasirishwa na maswali ya yule daktari.
“Hali ya wale wazee ndiyo kioo cha hali aliyokuwa nayo binti yao.”
“Dokta sijakuelewa,hebu nenda moja kwa moja kwenye pointi.”Denis alizidi kupaniki kutokana na maelezo ya yule daktari.
“Shaimaa yupo katika hali mbaya sana na kama jitihada zisipofanyika mapema anaweza akapoteza uhai wake.”Dokta alimpasulia Denis jipu alilolitaka.
“Unasema kweli dokta?”
“Ndiyo.”
“Kwahiyo unashauri nini kifanyike?”
“Anatakiwa ahamishiwe Muhimbili haraka iwezekanavyo ili kunusuru maisha yake.”Kutokana na mvunjiko alioupata Shaimaa,madaktari wa pale Bombo hospitali,walishindwa kuiunganisha miguu yake vizuri hivyo wakatoa ushauri wa kumhamishia mgonjwa huyo katika hospitali ya taifa Muhimbili iliyopo jijini Dar-es-salaam.
“Daah!ama kweli huu mtihani.”Denis alishusha mabega yake chini kwa unyonge.

“Tena mtihani mzito kweli kweli kwa wazazi wa huyu binti siyo kwako.Umewatia dosari ya maisha.Wameniambia kuwa huyo binti ndiyo tegemeo lao pale nyumbani.Wao hawana shughuli yoyote ya kuwaingizia kipato.Wamesema kuwa Shaimaa ndiyo alikuwa anatoka na kwenda kubangaizabangaiza mitaani na kuwaletea chochote kitu.Tangu mtoto wao apate ajali hawajaingiza chochote mdomoni na ukizingatia wanaishi na mabinti wadogo wawili wanaosoma.Wamekilaumu sana kitendo ulichomfanyia binti yao ambacho kimeathiri familia nzima.Kwahiyo kijana tambua kuwa laana ya wazee hao itakusumbua maisha yako yote.”
       ************
Je nini kitaendelea?Usikose kufuatilia mwendelezo wa hadithi hii iliyojaa visa na mikasa ya kusisimua.Nakutakia siku njema na Mungu akubariki sana.
     ********
Kwa maoni au ushauri napatikana kwa namba 0655089197/0766123623

Share this

Related Posts

Previous
Next Post »