STORY-PENZI LA MSHUMAA
MTUNZI-MZIRAY F.M.
SEHEMU YA 7
Ilipoishia sehemu ya 6
Baada ya Mzee Mwamba kuzungumza hayo kila mtu alitega sikio lake kusikiliza kauli ya Denis.Denis alinuua macho yake na kumtazama kila mmoja usoni halafu akatiisa kichwa kwa masikitiko. “Vivian.”Denis aliita kwa upole.
“Abee.”Vivian aliitikia huku akiwa na wasiwasi mkubwa moyoni.
“Nimeshakusamehe hivyo unaweza kurudi kwenu.”Baada ya Denis kutamka maneno hayo aliyatupa macho yake pembeni.
“Haah!sasa arudi kwao kivipi?”Winfrida alishindwa kumwelewa kaka yake.

Sasa endelea..........
“Kwani alivyokuja hapa si alisema amekuja kuomba msamaha!Ameshasamehewa sasa anasubiria nini hapa?”Denis alizidi kuwashangaza watu kutokana na maneno yake ya kejeli.
“Kwahiyo huyo ndiyo wifi yetu,siyo Shaimaa tena?”
“Mama unamuona Brenda anavyonitafuta?Brenda chunga mdomo wako nitakuja kukuharibu.”Kauli ya Brenda ilizidi kumtibua Denis aliyewaka kama moto wa mabua.
“Denis mwanangu,mbona hatukuelewi?Unasema kuwa umeshamsamehe Vivian halafu unamwambia aondoke!Inamaana unamfukuza mkwe wangu au?”Mama mtu aliamua kuvunja ukimya aliokuwa nao.
“Mkwe wako kivipi?”Denis alimtupia mama yake swali.
“Sasa kama umeshamsamehe Vivian maana yake si mkeo mtarajiwa!Ndiyo maana mimi namwita mkwe wangu.”
“Hivi mama mimi niwaeleze mara ngapi?Nimeshawaambia kuwa sitoweza kumuoa Vivian,mbona hamtaki kunielewa jamani!”Denis aliongea kwa jazba mbele ya wazazi wake.
“Hivi Denis umelogwa au?Tumeshakuambia huyu binti ndiyo mwenye sifa sahihi za kuwa mkeo.Unaenda kuhangaika na wasichana wa Tanga wa kazi gani?Sikiliza nikuambie,huyu ndiye mkwe wetu tunayemtambua huyo mwingine hatumjui.”Mzee Mwamba alizungumza kwa ukali baada ya kuona kuwa Denis hataki kuelewa.Hata hivyo Denis aliendelea kushikilia msimamo wake kama kawaida.Hakuvipa nafasi vitisho vya wazazi wake viweze kubadilisha maamuzi yake.
“Jamani!nyie ni wazazi wangu na ninapaswa kuwahishimu sana,ila kwa hili,mtanisamehe bure.Kama mnamtambua Vivian kuwa ndiyo mkwe wenu,endeleeni kumtambua hivyo hivyo lakini kwa upande wangu Shaimaa ndiyo kila kitu katika maisha yangu.Na kwa taarifa yenu nilichokifuata hapa ni kuwajulia hali sambamba na kuwaeleza kuwa natarajia kufunga ndoa na mchumba wangu wiki ijayo.Haijalishi kama mtanipa baraka zenu au hamtanipa.Haijalishi kama mtahudhuria kwenye harusi yangu ama la!lakini ndoa lazima ifungwe.”
Denis aliamua kutumbua jipu hadharani.Hakutaka kufanya kificho chochote,alieleza kitu alichopanga katika maisha yake ya ndoa.Baada ya kusikia hivyo,Vivian aliinama chini na kuanza kudondosha machozi ya uchungu.Alijutia alichokifanya ndani ya nafsi yake kwa kukurupuka bila kufanya uchunguzi wowote na matokeo yake ndiyo hayo ya kunyang’anywa tonge mdomoni.
“Haah!kaka,unafunga ndoa wiki ijayo bila hata kufanya maandalizi yoyote?”Winfrida alishtushwa na taarifa ya Denis.
“Hilo ni jibu unapigia mstari,siyo swali.Unataka nifanye maandalizi gani wakati nyie wote hapa mmenipinga?Sihitaji kamati wala sina haja na ndugu yeyote.Mkitaka mtakuja msipotaka basi.Kifupi ni kwamba,Shaimaa ndiyo ubavu wangu wa pili.Vivian akatafute mwanaume mwingine anayeona ni mwaminifu kuliko mimi.”Denis aliwaacha vinywa wazi wajumbe wote waliokuwepo kwenye kikao kile kisichokuwa rasmi.
“Lakini kaka…….”
“Lakini nini?Tena ninyi ndiyo msiniingilie kabisa maana mawifi mnasifika dunia nzima kwa kuharibu ndoa za kaka zenu.Kama mmeshindwa kuniunga mkono,sihitaji mazoea yoyote na nyie.Kuna hata siku moja mimi nilishawahi kuwafuata na kuwachagulia mwanaume?Shikeni hamsini zenu na mimi nishike zangu.”
Denis alizungumza kwa hasira mpaka mate yakamkauka mdomoni.Uso wake aliukunja kama Nyati akitamani kuwameza dada zake walioonesha kumpinga waziwazi.Kuona hiyo,Vivian aliinuka kwa hasira huku machozi yakifunika macho yake na kuamua kutoka nje ya nyumba ile.
“Vivian!Vivian!Wifi njoo unakwenda wapi?”
“Vivian mwanangu usiondoke.”
“Wifi njoo we ndiyo mwanamke wa nguvu hapa.”Bi Asma na wanaye wa kike walijaribu kumsihi Vivian aisondoke lakini tayari binti huyo alishafika nje.Brenda aliamua kumfuata na kumbembeleza lakini wapi!Hasira zilimkaba kooni akawa anazungumza kwa jazba.
“Sitaki!sitaki!Niache Brenda.Kaka yako ameshaamua kuoa hivyo mimi sina tena thamani katia familia yenu.Amekataa kunisamehe kwa kosa nililomfanyia ilihali nimeshamuomba radhi.Namtakia maisha mema katika ndoa yake,Mungu ambariki sana.”Baada ya Vivian kuzungumza maneno hayo kwa uchungu,alitoka mbio na kuyoyoma zake na kumwacha Brenda akiendelea kumwita bila mafanikio.
“Vivian!Vivian usiondoke jamani!Tutazungumza vizuri na Denis ataelewa tu.”Brenda aliishia kuzitazama nyao za Vivian ilihali mwili wa binti huyo haukuwepo eneo lile. “Unaona sasa kaka Denis ulichokifanya!Mtoto wa watu anakupenda yule sijui kwanini unamfanyia vitu vya ajabu namna hiyo?”Brenda aliporudi ndani moja kwa moja akaanza kumporomoshea lawama kaka yake.
“Naona nini?Mwache aende zake.Eti ananipenda!Angekuwa ananipenda angenisingizia huo ujinga wake?Anafikiri mimi ni malaya kama yeye.”
“Denis,maneno gani hayo ya kishenzi unazungumza mbele yetu?”Mzee Mwamba alikasirishwa sana na kitendo cha Denis kuropoka maneno yake yasiyofaa mbele ya wazazi wake.
“Lakini Denis ujue wivu ndiyo uliomfanya Vivian akuwazie vibaya juu ya uhusiano wako na Shaimaa.Siku zote mwenye mapenzi ya dhati kwako lazima awe na wivu juu yako.Hakukusudia kusema kwamba Shaimaa ni mpenzi wako.Ule ukaribu uliokuwa naye ndiyo uliomponza Vivian.”Brenda alijaribu kumtetea Vivian kwa Denis lakini wapi!
“Sikiliza nikuambie,tambua kuwa anayemuwazia mwenzie mabaya basi naye hufanya hivyo hivyo.”
“Si kweli.”Brenda alibisha.
“Hata kama usipokubali lakini ukweli ndiyo huo.Kwa kuwa alinisingizia mpaka akasema tuachane,nami nimeamua kufanya kweli na wiki ijayo nafunga ndoa na Shaimaa.”Denis aliendelea kushikilia msimamo wake.
“Hivi Dickson mwanangu unashindwa kuzungumza na ndugu yako na kumshauri kuwa huko anapokwenda anapotea.”Mama yake Denis aliamua kuvunja ukimya aliokuwa nao.Alimgeukia Dick aliyekuwa kimya muda wote na kumchangamsha kwa swali hilo.
“Nimeshazungumza sana na Denis lakini moyo wake umekuwa mgumu kubadilika.Ujue mapenzi yana nguvu sana na mtu akishapenda huwa hashauriki tena.Marafiki zake wengi tumemsihi mara nyingi tuwenzavyo lakini tumefua dafu.Sasa hivi tumekaa kimya na kuyapisha maamuzi yake yafanye kazi.”Dick aliongea maneno machache sana ili asionekane kama ni mpinzani kwa rafiki yake ilihali ameshakubali kuwa sambamba naye katika ndoa yake.
“Lakini huoni kama anapotea?”Mzee Mwamba naye aliamua kumuuliza Dick swali la mtego.
“Ha!ha!ha!ha!Ujue huyu ni mtu mzima na upeo mkubwa mno wa kufikiri.Ni msomi,anajua lipi zuri na lipi baya.Hivyo mimi sioni kama anapotea kwasababu yeye ndiyo mwamuzi wa mwisho na kila mtu huwa anajichagulia maisha yake mwenyewe.”
“Ha!ha!ha!ha!sisi tunaona unaegemea upande wake kwasababu ni rafiki yako.Hata kama mtu ana uhuru wa kujichagulia maisha yake mwenyewe lakini ushauri nao ni mzuri hasa ushauri wa wazazi katika kufanikisha malengo yake.”Safari hii Mzee Mwamba alizungumza kwa upole wa hali ya juu kitu kilimshangaza kila mtu mule ndani.
“Ni kweli kabisa kuwa wazazi ni muhimu sana katika maisha ya kijana wao hasa busara na hekima zao zinahitajika kwa kiasi kikubwa mno ili kufanikisha malengo bora ya mtoto.Hata hivyo,si kila ushauri wa wazazi huwa sahihi.Wakati mwingine inabidi kuwapa watoto nafasi ya kufanya maamuzi yao wenyewe.Kwa mfano katika suala hili la ndoa,Denis ndiyo ataenda kuishi na huyo mwanamke wake.Wala sisi hatutahusika kwa namna moja ama nyingine.
Japokuwa inasemekana kuwa wazazi wana maono ya kuona kitakachotokea mbele lakini mkimlazimisha Denis amuoe mwanamke ambaye hajamridhia,basi ndoa yake itakuwa ya mvurugano zaidi ya hii anayoitaka yeye.Hatoishi kwa raha kwa kuwa mwanamke aliyemuoa si chaguo lake bali ni la kwenu.Sasa hamuoni kama mtakuwa hamjamtendea haki hapo?”Kila mtu alizishangaa busara za Dickson.Hakuna mtu aliyeamini kama kijana huyo angeweza kuzungumza maneno yaliyoshiba hekima namna hiyo.Mara nyingi tumezoea kwamba wazee ndiyo wanaweza kutoa ushauri kama huo kuhusiana na masuala ya ndoa.
“Dickson.”
“Naam mzee.”
“Wewe umeoa?”Mzee Mwamba aliuliza kwa mshangao
“Hapana mzee wangu.”Dick alijibu kwa heshima.
“Yaani jinsi ulivyozunguza kwa ustadi wa hali ya juu utadhani upo kwenye ndoa zaidi ya miaka kumi.Hebu tuambie umeyapata wapi yote hayo?”
“Ha!ha!ha!ha!ha!”
“Ha!ha!ha!ha!ha!baba bwana.”
“Haaah!baba Denis mbona unamuuliza kijana wa watu maswali mengi hivyo?Au umekuwa polisi siku hizi?”Kila mmoja aliangua kicheko baada ya Mzee Mwamba kutaka kujua Dick alizipata wapi busara alizokuwa nazo.Bi Asma ndiyo aliamua kumtwanga mumewe swali kutokana na kuzidi kumwandama Dickson.
“Jamani!mimi nataka nijue tu!Kwani kuna ubaya kijana?”Furaha ilianza kuinyemelea ile nyumba taratibu baada ya vurumai la robo saa iliyopita kutulia.
“Ha!ha!ha!ha!hakuna ubaya wowote ule mzee wangu.Kwanza sitaki kuamini kuwa kama nina busara nyingi kiasi hicho.Ninyi wazee wetu ndiyo mna busara za kutosha kwasababu mmezaliwa muda mrefu na mmekumbana na changamoto za aina mbalimbali kushinda sisi.Hata hivyo suala la kuwa na desturi za kusoma vitabu mbalimbali linatujengea uwezo wa kujifunza mambo mengi.Ndiyo maana Mapadri wana uwezo wa kutoa ushauri ama kuwafungisha watu ndoa ilihali wao hawaoi.Yote hiyo ni kwasababu ya maarifa waliyoyapata toka vitabuni.”Elimu ya chuo kikuu aliyokuwa nayo Dick ndiyo iliyomwezesha kupambanua mambo vizuri namna hiyo.
“Ehee!umenikumbusha kitu.Sasa mwanangu umeamua kumuoa huyo binti wako wa Kitanga na kumkataa Vivian.Hiyo ndoa yenu inafungwa katika dini gani maana nakumbuka ulituambia kuwa Shaimaa hataki kubadilisha dini.”Mzee Mwamba aliuliza kwa shauku.
“Tumeamua kufunga ndoa mahakamani ili kila mtu abaki katika imani yake.”Denis alijieleza kwa kujiamini.
“Mahakamani!Hivi ndoa za mahakamani ni ndoa kweli?Sisi tumeshakuambia huyo binti hakupendi.Angekuwa na mapenzi ya dhati kwako lazima angekubali kufuata dini yako.Mwanangu,hapo umeruka majivu na kukanyaga moto.”Bi Asma alihamaki baada ya mwanaye kusema kuwa anakwenda kufunga ndoa mahakamani.
“Denis,hivi una kichaa?Sasa ndoa ya mahakamani ndiyo ndoa gani hiyo?”Winfrida naye aliamua kutia maneno yake.

“Sikilizeni niwaambie,suala la dini haliwezi kupima upendo alionao mtu kwa mchumba wake.Mnaweza mkaoana watu wa dini moja na msielewane.Au kama mnaona hiyo ni mbaya mimi nipo tayari kubadilisha dini ili tuwe kitu kimoja.”
                                        *********
Je nini kitaendelea?Tukutane Jumatano ijayo tuweze kuendeleza hadithi hii iliyojaa visa na mikasa ya kusisimua...Nakutakia siku njema na Mungu akubariki sana.
                                           ***********
Kwa maoni au ushauri napatikana kwa namba 06555089197/0766123623

Share this

Related Posts

Previous
Next Post »

2 comments

comments