STORY-PENZI LA MSHUMAA
MTUNZI-MZIRAY F.M.
SEHEMU YA 10
Siku hiyo Denis alikuwa uwanja wa ndege wa Mwalimu Julius Kambarege Nyerere akisubiria ndege ielekeayo Tanga.Safari yake haikuwa ya Tanga tu bali alitaka pia kwenda Kenya katika bandari ya Mombasa kushughuli gari lake lililokwama katika bandari hiyo.Baada ya tangazo kutolewa juu ya abiria wa Tanga,Denis alimgeukia mchumba wake na kumkumbatia huku akimpiga mabusu moto moto ya kumuaga.
“Usijali Vivian wiki ijayo nitakuwa hapa.Nitakwenda kwanza Mombasa mara moja kuitoa ile gari yangu na baada ya hapo nitarejea Tanga katika shughuli zangu nyingine zilizonipeleka huko.Nikimaliza nadhani sitakuwa na sababu yoyote ya kuendelea kukaa huko bila kazi ya msingi.”Denis alizungumza kwa hisia za mapenzi.
“Mmmmh!nitakumisi sana mpenzi wangu.Wiki moja ni ndefu sana kwangu.”Vivian alieleza hayo huku akimpigapiga Denis mgongoni.
“Ha!ha!ha!ha!ha!jamani wiki moja ndefu!Mmmmh!Vivian umezidi.”
“Siyo hivyo Denis,ujue nimezoea kuonana na wewe kila siku.Ikipita siku moja tu sijakuona nahisi homa.Sembuse hiyo wiki moja si nitakufa kabisa.”
“Ha!ha!ha!ha!ha!usijali Vivian muda si mrefu tutafunga ndoa na utakuwa na mimi mpaka utanichoka.”Denis aliendelea kumpa moyo mchumba wake waliopanga kufunga ndoa miezi michache itakayofuata.
“Ha!ha!ha!ha!nikuchoke kwa kipi?Wala siwezi kukuchoka mpenzi wangu hata siku moja.Tena kipindi hicho ndiyo nitakuwa mke halali wa bwana Denis,watanikomaje!”Vivian alizungumza kwa kujiamini katikati ya kumbatio la Denis.Baada ya kuagana Denis alivuta begi lake dogo la matairi na kuelekea katika ndege na hiyo ni baada ya kukaguliwa.Alipofika kwenye mlango wa ndege aligeuka na kumuona Vivian akiwa bado kasimama anamwangalia.
Alinyoosha mkono wake na kumpungia ambapo Vivian naye alimjibu kwa kumpungia pia.Baada ya hapo Dens aliingia ndani ya ndege na baada ya nusu saa ndege iliacha ardhi ya Dar-es-salaam na kupaa angani.Alifika Tanga majira ya saa 6 mchana ambapo alikodi tax na kuamuru apelekwe katika hoteli ya Dolphin iliyopo maeneo ya Kwaminchi karibu na barabara ielekeayo kwa mkuu wa mkoa.
Mara kwa mara Denis alipokwenda Tanga alipenda kufikia katika hoteli hiyo ama hoteli nyingine iliyopo jirani yake inayoitwa Nyinda hoteli.Hoteli hizo zilisifika katika kutoa huduma bora za malazi na vyakula ndani ya Jiji hilo la Tanga.Baada ya Denis kupata chakula aliamua kuoga na kupumzika.Alichukua simu yake na kumpigia Vivian kumjulisha kuwa amefika salama na kwa muda huo yupo hetelini anakula kiyoyozi.Waliongea kwa kirefu sana mtu na mchumba wake wakati dakika chache tu zilizopita walikuwa pamoja Jijini Dar-es-salaam.
Baada ya simu kukatika Denis aliuchapa usingizi hadi jioni.Alipoamka aliamua kuusawiri mji wa Tanga kwa kuzungukazunguka maeneo tofauti tofauti ndani ya Tanga mjini.Giza lilipoanza kumeza jiji hilo,Denis alirejea hotelini na kutulia.Alipanga kwenda Mombasa siku inayofuata kulitoa gari lake katika bandari ya mji huo.
Kesho yake asubuhi Denis aliondoka kuelekea Mombasa akiwa ndani ya basi la kampuni ya Tahmed.Walipofika Horohoro mpakani waliingia kwenye jengo la uhamiaji na kufuata taratibu zote ikwemo kukaguliwa hati za kusafiria kisha wakaruhusiwa kuendelea na safari.Walipofika Mombasa Denis hakutaka kupoteza muda.Alikwenda moja kwa moja hadi bandarini na kumalizana nao ambapo alifanikiwa kulitoa gari lake aina ya Range Rover majira ya saa 12 jioni.
Kwa kuwa muda ulikuwa umekwenda sana basi Denis akaamua kuchukua hoteli moja ya kifahari na kulala ili kesho yake aanze safari ya kurejea Tanga.Ilipofika asubuhi Denis aliingia ndani ya gari lake na kuanza kukanyaga mafuta kuelekea Tanga.Alipofika Horohoro mpakanni kama kawaida alikaguliwa na alitakiwa kuingia TRA kwaajili ya malipo ya gari lake.Baada ya kila kitu kukamilika aliendelea na safari kwa mwendo wa kasi.Moyo wake ulifurahi sana kufanikisha kilichompeleka huko kwani gari alilokuwa analihusudu sasa lipo mikononi mwake.
Alipofika Tanga kabla hajaingia hoteli aliyofiia,Denis alielekea sheli iliyopo maeneo yale ya Kwaminchi na kujaza mafuta.Baada ya kutoka hapo alianza kurejea taratibu ili akapumzike.Wakati akiwa anaendesha gari mdogo mdogo mbele yake kulikuwa na pikipiki iliyokuwa inaendeshwa kwa kasi ya ajabu huku kukiwa na binti aliyepakizwa nyuma.Kabla hawajafika maeneo ya reli ghafla yule binti aliponyoka toka katika pikipiki ile baada ya kugonga jiwe lililokuwa linazagaazagaa barabarani na hatimaye akadondoka chini.
Denis alishuhudia pikipiki nyingine ikimvaa yule binti na kumtupa pembeni.Wale madereva wa pikipiki zote mbili waliyumba barabara nzima na kusababisha ajali ya magari mengine yaliyokuwa yanawakwepa.
Kwa bahati nzuri walifanikiwa kuzimudu pikipiki zao na kukaa sawa ambapo ili kuepuka lawama juu ya kile kilichotokea walivuta mafuta na kutokomea eneo lile kwa mwendo mkali.Watu walikusanyana kumshuhudia yule binti aliyekuwa ameumia vibaya mno.Raia wawili waliamua kupiga mkono gari ya Denis na kumwomba amwahishe yule binti hostipali akapate matibabu ya haraka.Kutokana na uchungu alioupata Denis baada ya kushuhudia ajali ile,aliamua kupaki gari pembeni na kutoa msaada wake.
Binti alipakiwa kwenye gari kisha Denis akapiga moto kumwahisha katika hospitali ya Bombo iliyopo karibu na maeneo ya Raskazoni.Alipofika katika hospitali hiyo walikataa kumpokea mgonjwa kwasababu hakuwa na kithibitisho chochote toka polisi kinachoonesha kuwa msichana huyo alipata ajali.
“Sasa jamani si mtoe hata huduma ya kwanza!Inamaana hamuoni jinsi mtu alivyoumia anavuja damu miguu yote?Masuala ya polisi si yatafuata baadae.”Denis aliwafokea wale madaktari wa hospitali ile baada ya kugoma katakata kumpokea mgonjwa kabla hajapitia polisi.
“Kijana hapa tunafuata utaratibu uliopangwa.Hatuwezi kumpokea huyo binti mpaka uwe na kibali toka polisi.”Daktari mmoja alimpa Denis maelezo hayo huku akiendelea na shughuli zake.
“Mnasema mnafuata utaratibu wakati mtu anakufa hapa!Kwahiyo ni afadhali mtu afe kuliko kuvunja huo utaratibu?”Denis aliuliza kwa hasira.
“Kijana haina haja ya kupaniki.Kituo cha polisi wala hakipo mbali sana ni hapo tu Raskazoni.Ni bora uende hapo mara moja ili mgonjwa wako aje kupata matibabu haraka.”Denis hakuwa na jinsi,aligeuza gari na kuelekea kituo cha polisi cha Raskazoni.Baada ya kutoa maelezo yake walimwandikia kibali cha kutibiwa na kurudi tena hospitali.


“Si unaona sasa ulivyorahisisha kazi.Ungeendelea kulumbana na sisi mgonjwa wako si angekufa?Kama tungemtibu hivyo hivyo halafu akatufia tungeijibu nini serikali?”Daktari mwingine alizidi kumtia hasira Denis aliyekuwa anavuja jasho mwili mzima kama mtu aliyemwagiwa maji.
“Mchukueni mgonjwa acheni porojo.Nyie vipi?mbona mnakuwa kama siyo wasomi vile!”Denis alipaniki akaanza kuwafokea kwa hasira huku mgonjwa akiwa bado mikononi mwake.Kitanda cha magurudumu kililetwa na yule msichana akapakizwa juu ya kitanda hicho na kusukumwa na wauguzi kuelekea hodini.Denis alipojitazama,nguo zake zilikuwa zimechafuka damu kila mahali kutokana na kumbeba yule binti aliyekuwa anavuja damu miguuni.
Alifanya zoezi hilo alipokwenda polisi na pia aliporejea pale hospitalini kwasababu alikuwa peke yake.Wale wananchi waliomsimamisha na kumuomba msaada,baada ya kumpakiza yule binti kwenye gari hakuna hata mmoja aliyejumuika naye kuelekea hospitali.Kutokana na hilo,Denis alifanya kila kitu mwenyewe ikiwemo kumfungulia huyo binti faili la matibabu.
“We kaka mgonjwa wako anaitwa nani?”Denis aliulizwa swali na nesi mmoja aliyekuwa pale mapokezi.
“Mimi sifahamu anaitwa nani kwasababu nimeombwa tu na wananchi nimlete hapa baada ya kupata ajali hivyo sifahamu chochote kuhusu yeye.”Denis alipoeleza kuwa hamjui huyo  msichana na wala hafahamu anapoishi,ilizua utata kidogo.
“Unasema humfahamu!humfahamu kivipi?We si ndiyo umemleta hapa?”Yule nesi alishindwa kumwelewa kabisa Denis.
“Sasa hapo dada yangu usichokielewa kitu gani?Nimeshakwambia huyo binti mimi simfahamu.Nimeombwa tu msaada wa kumleta hapa baada ya kupata ajali ya pikipiki pale maeneo ya Kwaminchi kabla hujafika mjini.”Denis alijitetea.

“Kwahiyo hapa kwenye faili lake tuandike nini?”Yule nesi alizidi kumwandama Denis.

                        *******
Je nini kitaendelea?Usikose sehemu ijayo ya mwendelezo wa stori hii..Nakutakia siku njema
                       *******
Kwa maoni au ushauri napatikana kwa namba 0655089197/0766123623

Share this

Related Posts

Previous
Next Post »