STORY-PENZI LA MSHUMAA
MTUNZI-MZIRAY F.M.
SEHEMU YA 16
Ilipoishia sehemu ya 15
“Basi Denis usilie mpenzi wangu.Haya mambo tutayamaliza tukishatoka hapa.Tutazungumza kwa kirefu na wazazi wa huyu binti tujue tunamalizana vipi nao ili turudi Dar-es-salaam.”Vivian alimfuta Denis machozi na kumwambia akaze moyo yeye ni mtoto wa kiume.Alimshika mkono na kusogea naye karibu na kitanda cha Shaimaa.

Sasa endelea.....
“Habari yako binti?”Denis alimjulia hali Shaimaa.
“Kwa kweli hali yangu siyo nzuri hata kidogo.Madokta wamesema naweza nikakatwa miguu.Uuwiii!jamani eeh!Mimi nimeshakuwa mlemavu wa kudumu milele na milele.Nitaishije mimi na ujana huu?”Shaimaa alizungumza huku akiwa anamwaga machozi mfululizo.Kila mtu aliguswa na maneno yake ya uchungu.Hadi Denis aliyekuwa na hasira naye kutokana na kumsingizia kesi isiyomhusu,huruma ilimwingia.Wakati wakiwa katika hali ya huzuni mara nesi akaingia na kuwaambia kuwa muda wa kumwona mgonjwa umekwisha hivyo waondoke warudi tena kesho yake..
Walipotoka nje Denis alibadilishana namba za simu na wazazi wa Shaimaa kisha wakaondoka zao.Baada ya hapo Denis naye akaingia kwenye gari na kuwaomba ndugu zake wampeleke hoteli aliyofikia ambayo ni Dolphin hoteli akapumzike.Hapakuwa na umbali wowote toka Bombo hospitali hadi maeneo ya Kwaminchi ilipo hoteli hiyo.Baada ya kuingia hotelini Denis alienda bafuni na kujimwagia maji kisha akaenda kupata chakula akiwa sambamba na ndugu zake.Wakati wakiwa wanaendelea kupata chakula cha usiku,Denis aliwasimulia jamaa zake jinsi ajali ya Shaimaa iliyotokea mpaka raia wakamsimamisha na kumwomba amwahishe binti huyo hospitali.
“Haaa!kwahiyo yeye aligongwa na pikipiki?”Brenda aliuliza kwa mshangao.
“Ndiyo ilivyokuwa na madereva wa pikipiki zote walifanikiwa kutoroka eneo lile.Nashangaa nilipofika hospitali yule msichana akanigeuzia kibao na kusema kuwa eti mimi ndiyo nimemgonga.Sijui ni kwanini ameamua kufanya hivyo?”Denis alizungumza huku akiwa anakata msosi haraka haraka kwani tangu jana yake alipokumbana na mkasa huo hakuingiza kitu chochote tumboni.
“Ana haja eti!tena siyo haja ndogo,ni haja kubwa ya wiki nzima.Kama kwao hawana choo atafute pori akajisaidie.Nyoo!anataka kuponea kupitia migongo ya watu.”Winfrida alikasirishwa sana na kitendo alichofanyiwa kaka yake.Alianza kubwabwaja maneno yake kuntu utadhani aliyekuwa anamwambia alikuwa eneo lile.
“Sijajua ana lengo gani hasa na mimi?”Denis alijisemea.
“Labda anakutaka.”Brenda aliropoka huku akiwa anamtupia Vivian jicho la machale.
“Mbona unaniangalia kwa wasiwasi hivyo wifi?”Vivian alimuuliza Brenda baada ya kumwona akimsorora kwa jicho la pembeni.
“Usije ukanirukia bure.Denis ni wako hachukuliwi na mtu yeyote.Kwahiyo Denis wewe umechukua uamuzi gani juu ya suala hilo?Upo tayari kuhudumia mzigo usiokuhusu?”Baada ya Denis kuulizwa swali hilo na mdogo wake,aliacha kula na kumtazama halafu akatikisa kichwa kwa masikitiko.
“Kwa kuwa nimeshajifunga mwenyewe kwa kusaini zile karatasi za polisi itabidi  nimhudumie tu huyo binti mpaka atakapopona.Halafu baad……….”
“Mmmh!mwenzangu una hela za kuchezea.Kugongwa agongwe na mwingine halafu wewe ndiyo uhudumie!Kaka yangu hapo umeliwa wala sikushauri.Tuna uwezo wa kulipeleka shauri hili mahakamani na maamuzi mazuri yakatolewa.Wale ni polisi tu hawana lolote.Tuliamua kukushauri usaini ili tu utoke katika mazingira yale lakini kwa kweli sihafikiani na hilo suala hata punje.”Maneno ya Denis yalikatizwa na mdomo wa Brenda aliyeanza kuongea kama cherehani.Alipingana kabisa na maelezo ya kaka yake ya kutaka kumhudumia Shaimaa kama alivyosaini na kukubaliana na masharti ya dhamana.
“Hata mimi mwenyewe nipo upande wa Brenda.Haiwezekani utoe pesa zako kumhudumia mtu aliyekusingizia kosa kama hilo.Msaada wako wa kumpeleka hospitali unatosha kabisa.Halafu hana hata aibu,eti anajilizaliza mbele yetu kinafki.Anafikiri tungemchekea hivi hivi!Hajui kama amekuingiza matatizoni au?Yule siyo mtu,hana ubinadamu hata kidogo.Au unasemaje wifi?”
“Tupo pamoja.”Vivian aliungana na wifi zake watarajiwa kumpinga Denis kutokana na maamuzi aliyotaka kuyachukua.
“Acheni tu nimhudumie,kwani itagharimu shilingi ngapi?Si itakuwa tu  pesa ya mboga kwangu ndiyo imetumika!Naamua kufanya hivyo ili nijue huyo binti ana nia gani hasa na mimi.Nafikiri akishapona ataweza kuzungumza vizuri.”Siyo kwamba Denis hakuchukia ushenzi aliofanyiwa na Shaimaa la hasha!Alichukia tena zaidi ya sana ikafika hatua chuki ikajipandikiza ndani ya moyo wake juu ya binti huyo.Lakini alijitolea kumhudumia ili awe karibu naye na mwishowe iwe rahisi kwa yeye kujua lengo lake la kumsingizia hiyo kesi.
Alifikiri pengine huyo binti anamfahamu na isingekuwa rahisi kiasi kile kuthubutu kumsingizia mtu asiyemjua hata kidogo kesi kubwa namna ile.Pengine kama si hivyo,Denis alitaka kujua ni kita gani kilichomsukuma kufanya hivyo.Majibu ya vyote alivyokuwa anajiuliza hawezai kupata kwa mtu mwingine yeyote yule zaidi ya Shaimaa.
Ndiyo maana alikubali kuibeba dhamana ile japokuwa mwanzoni aliipinga katakata,ili tu ajue mengi toka kwa binti huyo.Kila mtu alijaribu kumpinga lakini Denis alishikilia maamuzi yake na kuwaambia kuwa yeye ni mtu mzima anajua anachokifanya.
Baada ya kulumbana kwa muda mrefu mwishowe wakaamua kusalimu amri.Denis alikubali kuubeba mzigo ule akiamini kuwa Mungu atamlipa binti huyo kwani malipo ni hapa hapa duniani.Vile vile aliamini pengine hilo ni jaribu la Mungu kwake ili amwone kama ana uwezo wa kutoa msaada kiasi gani kwa wengine hata kama ni maadui zake.
Baada ya kumaliza kula walikwenda mapokezi kwa lengo la kupata vyumba kwaajili ya kulala.Kwa bahati mbaya waliambiwa vyumba vimejaa hivyo ikawalizimu kwenda kulala hoteli ya jirani inayojulikana kwa jina la Nyinda hoteli.Dick na Dolan walichukua chumba kimoja na Winfrida pamoja na Brenda nao wakachukua chumba kimoja.Vivian yeye alikwenda kulala na Denis pale pale Dolphni hoteli.
Wakati huo huo Denis alishazungumza na wazazi wake na kuwaambia kuwa ameshamalizana na polisi juu ya sakata hilo.Aliwataka ndugu zake warejee Dar-es-salaam wakaendelee na shughuli zao kwa kuwa yeye tayari yupo huru.
“Sasa Denis ulivyosema kwamba sisi turudi nyumbani wakati hali yako bado haipo vizuri unamaanisha nini?”Vivian alimuuliza Denis wakiwa kitandani huku akichezea kidevu cha mwanaume huyo.
“Ha!ha!ha!ha!usiwe na wasiwasi mpenzi wangu.Kwa sasa hivi nina hali nzuri tu.Hata ninyi wenyewe mliniambia cha muhimu ni kuwa huru kwanza halafu mambo mengine ndiyo yafuate.Nilichokuwa nakifuata Tanga bado sijakikamilisha.Sijatembelea ofisi yangu hata moja kwahiyo kazi hiyo nataka nianze kuifanya kesho.Akina Dick wameacha ofisi hazina msimamizi hata mmoja.Akina Brenda nao wana shughuli zao na wewe pia hivyo hivyo.Sasa mtakaa na mimi hapa halafu kazi zenu mmwachie nani?”Denis alizungumza na mchumba wake kwa sauti a upole.
“Basi wao warudi halafu mimi nibaki.”Vivian alikuwa na kaugumu fulani ndani ya moyo wake.Hakutaka kuamini kama mpenzi wake ataweza kugangaika mjini peke yake ilihali bado hakuwa vizuri kiafya.
“Vivian,najua unanipenda sana na kunijali kuliko maelezo.Lakini pamoja na yote hayo hatuwezi kukaa pamaoja kila wakati halafu kazi zidorore.Huu utakuwa ni uzembe wa hali ya juu sana.Nashukuru mmekuja kuniona na kunifanikiwa kunitoa ndani.Sasa kinachoktakiwa ni kurudi makazini jamani!”
Denis alikuwa ni mwanaume mchapa kazi kila dakika.Hakupenda vitu vidogo vidogo vimpotezee wakati wake wa kuwajibika.Aliamini uwepo wa Vivian eneo lile litaathiri ufanisi wake wa kazi kwani muda wote itakuwa ni mapenzi tu badala ya kufanya kilichompeleka Tanga.Ndiyo maana aling’ang’ania watu warudi katika shughuli zao za uzalishaji mali.
“Najua unanilazimisha niondoke ili upate muda mzuri wa kumhudumia yule msichana.”Vivian alianza kuyapeleka mawazo yake mbali kabisa.
“Unamaanisha nini kusema hivyo?”Denis aliuliza kwa mshangao.
“Amna,kawaida tu.”Wivu ulianza kutafuna Vivian akiamini kuwa Denis anafahamiana na Shaimaa hivyo anamuondoa pale Tanga ili iwe rahisi kufanya mambo yake na msichana huyo aliyekuwa hoi kitandani.
“Haya,kama umeshaanza kuwaza vitu vingine ambavyo havipo,hiyo ni shauri yako.Unajipa presha za bure bila sababu ya msingi.Tambua kuwa nakupenda sana kuliko mwanamke yeyote yule ndani ya dunia hii.Wewe ndiyo ua la moyo wangu.Wewe ndiyo chakula cha moyo roho yangu.Wewe ndiyo kioo changu,ndiyo muongozo wangu.Wewe ndiyo kila kitu katika maisha yangu.Unapaswa kujiamini unapokuwa na mimi au unapokuwa mbali nami.”
“Haya baba nimekusikia.”Vivian alimjibu Denis kisha akageukia ukutani na kulala.Denis alibaki na mawazo juu ya hali ile iliyoionesha mchumba wake.

“Mmmh!huyu msichana huwa ana wivu sana.Sijui ni kwanini huwa ajiamini katika mapenzi.Nakumbuka kipindi kile kabla hajawafahamu akina Brenda alifikiri ni wasichana wangu.Nashangaa tena sasa hivi ananiambia habari za yule msichana mgonjwa!Kwahiyo anataka kuniambia na yule ni mwanamke wangu!Vivian punguza wivu bwana,utakuja kujiua bure!”

Baada ya mawazo hayo kuanza kupotea ndani ya kichwa cha Denis,taratibu usingizi ukaanza kumnyamelea mdogo mdogo.Hakujua hata amelala saa ngapi lakini alikuja kushtuka baada ya kudondokewa na matone ya maji baridi usoni.Alipofungua macho yake alimuona Vivian akiwa na glasi ya maji mkononi.

                *********
Itaendelea....Asante kwa ufuatiliaji wako wa hadithi hii.....Mungu akujalie afya njema.Nakutakia siku njema.
          *******
Kwa maoni au ushauri napatikana kwa namba 0655089197/0766123623

Share this

Related Posts

Previous
Next Post »