STORY-PENZI LA MSHUMAA
MTUNZI-MZIRAY F.M.
SEHEMU YA 14
Ilipoishia sehemu ya 13
“Unaona sasa!We unadhani Range Rover ni milioni ngapi? Sasa mtu kama wewe utasingiziwa kesi gani?Utaambiwa umeiba kuku kama sisi?Kesi zenu ndiyo hizo za kugonga watu kwa magari yenu,kupiga au kuua binadamu wenzenu.Sasa utasemaje umesingiziwa!”       Kila mtuhumiwa ndani ya mahabusu ile alimwandama Denis.
“Hana lolote huyo ni mnafiki tu.Asingiziwe wapi!Ameamua kumpanda dada wa watu  miguuni na Range lake.Bora ufungwe tu uwe sawa na sisi.”

Sasa endelea......
“Kweli kabisa,bora tufanane tu.Hawa huwa wanapeana ajira wenyewe.Utakuta ofisi yake wamejazana ndugu chungu nzima.Nenda wewe sasa utaambiwa una vyetu vizuri lakini hakuna ajira.”Denis alitengwa na kila mtu ndani ya lokapu ile.Wengi wao waliochukizwa naye ni vijana wenye umri sawa na yeye na wachache sana waliomzidi.
Hawakupenda kijana mwenye umri sawa na wao awe na mafanikio kiasi kile ilihali wao walikuwa wanasota mitaani kutokana na ugumu wa maisha.Walitiwa mbaroni baada ya kujiingiza kwenye makundi ya kihuni na kupora mali za watu.
Hawakutaka kujituma katika kufanya kazi ili wajipatie kipato chao cha halali.Wanaisingizia serikali kwa kutowapa ajira.Fursa za ajira mbona zipo chungu nzima sema vijana hawataki kuzichangamkia.Pengine labda hakuna mazingira rafiki yatakayowasukuma kufanya mambo ya maendelea.
Lakini kwa vijana waliofanikiwa kama Denis wao waliwezaje?Si walikazana katika kufanya kazi kwa bidii na mwisho wake matunda yanaonekana.Uvivu umewajaa vijana wengi wa nchi hii ndiyo maana hawapati maendeleo.Hawataki kufanya kazi wanaishia kukaa vijiweni na kupiga zogo tu.Wanabaki kuwapiga majungu wenzao waliofanikiwa.Badala wajifunze toka kwa watu hao wanabaki kusema mali zao siyo za halali.Mara yule alimtoa mama yake kafara ndiyo maana ni tajiri vile.Mara huyu anafuga mandondocha ndani ya nyumba ndiyo maana ana mali chungu nzima.Mtaendelea kusema mali za wenzenu tu lakini wao wanazidi kusonga mbele.
“Jamani inawezekana kweli kasingiziwa tusimpinge moja kwa moja.”Mtuhumiwa mmoja alijitokeza na kuwa upande wa Denis baada ya kuona wenzake wamemwandama sana kijana huyo.
“Haa!huyu anasema nini?
“Mimi mwenyewe namshangaa.”
“Wewe unamtetea huyu unamjua?Unafikiri akitoka hapa atafanya mipango ya kukutoa humu ndani?Hizo ni ndoto za alinacha kaka.”
“Huyu jamaa kagonga kweli,wewe unatetea nini?”
“Nyie mmemuona akimgonga huyo msichana?Kama amesingiziwa tu kisa kamuona jamaa ana hela ili alipwe!Acheni hiyo,haya mambo ya kusingiziwa yapo kwa mtu yeyote bila kujali kipato chake.Omba tu Mungu yasikukute maana utahisi umetengwa na dunia nzima.”Yule jamaa kweli alidhamiria kumtetea Denis.
“Mbona unamtetea sana?Huyu jamaa ndugu yako nini?”
“Siyo ndugu yangu ila nawapa makavu.Acheni kumwandama mtu bila sababu ya msingi.Sisi wote tupo humu ndani ni wa moja.Haina haja ya kuanza kuleta matabaka ilihali wote tupo kwenye matatizo.”Kweli jamaa aliamua kumkingia Denis kifua.
“Kwani wewe unasemaje?”
“Kuhusu nini?”
“Chochote kile.”Wale watuhumiwa wengine baada ya kuona kuwa Denis kapata mtetezi wakaanzisha vurumai ndani ya mahabusu.
Denis pamoja na yule kijana aliyekuwa upande wake walipigwa sana mpaka wakaanza kuvuja damu.Askari walipokwenda kutuliza ile vurumai hawakuchagua wa kumpa kisago.Walisambaza mkong’oto mahabusu nzima bila kujali aliyeanzisha ugomvi wala aliyepigwa.
Masikini ya Mungu,Denis aliumia vibaya mno maeneo ya usoni.Alipasuka paji la uso na upande wa kushoto karibu na shavu.Alivuja damu uso mzima.Vile vile macho yake yote mawili yalivimba sana baada ya kupigwa ngumi za usoni.Denis alijigaragara chini kutokana na maumivu makali aliyokuwa anayasikia.Moyoni mwake alimlaani yule msichana aliyemsingizia kesi isiyokuwa ya kwake.
Matatizo anayoyapata yametokana na kauli ya Shaimaa kwamba Denis ndiyo kamgonga na kumvunja miguu yake yote miwili wakati haikuwa hivyo.Denis alilia sana akawa haamini kama kweli ipo siku ambayo angekuja kutumbukia kwenye shimo lenye miba mikali namna hiyo.Hakujua atatoka lini ndani ya chumba kile kilichotawaliwa na giza totoro pamoja na ufinyu wa hewa.
Alizoea kulala katika chumba cha kisasa juu ya kitanda cha sita kwa sita.Lakini siku hiyo alijibanza kwenye kona karibu na ndoo ya kinyesi iliyochanganyika na mikojo ya watuhumiwa wenzake.Harufu iliyokuwa inatoka katika ndoo hiyo iliumiza sana pua yake.
Alijaribu kukabiliana nayo lakini wapi!Alipiga chafya mfululizo kama beberu.Pia kulikuwa na joto kali sana kutokana na mrundikano wa watu wengi katika chumba kidogo kama kile.Watuhumiwa walipata shida mno lakini hawakuwa na namna nyingine ya kuepukana na hatari hizo.Siku hiyo iliyoyoma bila Denis kufunga jicho lake mpaka asubuhi.Kesho yake asubuhi majira ya saa tatu Denis alitolewa kule mahabusu na kuingizwa chumba cha mapokezi.
“Kijana umeona maisha ya humo ndani yalivyokuwa matamu?Kwa taarifa yako utakaa huko mwezi mzima kama hautotupa maelezo ya kueleweka.”Yule askari mpelelezi aliutonesha moyo wa Denis kwa maneno yale ya kejeli.
“Sasa afande unataka nikupe maelezo gani mengine ya ziada?Mimi nimeshawaambia kuwa sjamgonga yule binti.Kapimeni basi gari yangu muone kama kweli imefanya tukio hilo.”
“Gari tumeshaipima na majibu ndiyo hayo.Wewe ndiyo uliyehusika na ajali hiyo.”
“Hivyo vipimo vyenu siyo sahihi.”Deni alipingana na maelezo yale.
“Kijana chunga sana.Kwahiyo mimi afisa mzima wa polisi ni muongo?Badala ya kuwa mpole ili nikusaidie,wewe unaleta jeuri!Hii kesi ikienda mahakamani lazima ufungwe na biashara zako zitaharibika.”Yule askari alianza kujikombakomba kwa Denis kwa lengo la kumsaidia.Denis aliinua uso wake na kumtazama askari yule aliyekuwa anajizungusha katika kiti chake.
“Kwahiyo wewe unataka kunisaidiaje?”Denis aliuliza kwa upole.
“Hayo ndiyo maneno sasa.Mimi sihitaji pesa yako hata kidogo.Nataka nikufanyie mpango wa dhamana ili utoke humu ndani.”
“Ninachofahamu mimi,dhamani ni haki yangu ya msingi.Sasa utasemaje kwamba wewe ndiyo wa kunifanyia mpango wa dhamana!”Denis alijaribu kujitutumua.
“Sikiliza nikuambie kijana,hapa duniani hakuna haki,haki ipo mbinguni.Sasa wewe neng’eneka kama hujaozea jela na pesa zako.Wewe unadhani pesa zinaweza kufanya kazi kila sehemu?Usiishi kwa kukariri utakufa.Shenzi kabisa!Haki haki,ungekuwa na haki ungekuwepo hapa?Hebu fungua akili yako,siyo kila kabila linachezewa kijana.Hii ndiyo Tanga waja leo waondoka leo.Tanga raha bwana.”Taarabu alizoimbiwa na yule askari zilimshangaza sana Denis.Ilibidi awe mpole ili ajue jamaa anataka nini toka kwake.
“Haya niambie utanisaidiaje afande?”
“Nipe namba za simu za ndugu yako yeyote yule nizungungumze naye ili afike hapa kituoni kwaajili ya dhamana.Suala la masharti ya dhamana hiyo utayafahamu atakapofika huyo ndugu yako.”Denis alitakiwa kutoa namba  za simu ili mawasiliano yafanyike aje kutolewa dhamana.
“Katika orodha ya majina yaliyopo kwenye simu yangu kuna jina la Dick.Mpigie huyo mweleze yote yaliyonisibu.Nadhani atakuja kunitolea hiyo dhamana.”Baada ya Denis kutoa maelezo hayo alirudishwa lokapu na kutulia.Alishindwa kuelewa yule askari ana lengo gani na yeye.Hata kama anataka kumsaidia lakini kwanini ampe maneno ya kejeli kama yale.Hali hiyo ilizidi kumweka njia panda.
Mchana nao ukakatiza bila kulishibisha tumbo la Denis kama ilivyokuwa asubuhi.Minyoo walipiga miayo mfululizo ndani ya tumbo kuashiria kuwa walihitaji chochote kitu.Hata hivyo Denis alishindwa kupambana na wazoefu wa mahabusu ile ili kupata chakula kidogo kilichokuwa kinagawiwa.Ilipofika jioni majira ya saa 11 Denis alichukuliwa tena na kupelekwa katika chumba cha mpelelezi.Alipofika ndani ya chumba hicho hakuamini macho yake kwa kile alichokiona.
Mbele yake alisimama Dickson na Dolan huku kwenye viti vya upande wa kushoto waliketi wadogo zake,Brenda na Winfrida.Upande wa kulia aliketi mchumba wake pamoja na wazazi wa Shaimaa.Walipomuona tu Denis katika hali ile kila mmoja alihamaki kivyake kuonesha machungu aliyoyapata.
“Mamaaa!Mungu wangu!Denis!Denis mchumba wangu nini kimekupata?Niambie Denis,niambie!”Vivian aliinuka na kwenda kumkumbatia Denis kwa nguvu huku machozi yakimtoka.
“Jamani mmemfanya nini kaka yetu Denis?Kwanini mmempiga?Masikini kaka Denis ameharibika uso mzima.”
“Uuuwi!Denis jamani eeeh!Umefanya nini kaka yangu?”Brenda na Winfrida nao hawakubaki nyuma.Walianza kuangua vilio baada ya kuyaona mabadiliko aliyokuwa nayo kaka yao.Dolan na Dick aliugulia kimya kimya ndani kwa ndani.Si uanjua uwanaume ni kujikaza,basi walijikikaza kisabuni lakini moyoni mwao walihuzunishwa sana na hali ya rafiki yao ambaye ndiyo bosi mkuu katika kampuni yao ya mafuta.
“Shenzi!tulieni wote!Hii siyo kliniki bali ni kituo cha polisi.Kuna kanuni na taratibu zake hivyo zinapaswa kuheshimiwa na kila mtu.Nani kawaruhusu kulia?Binti nenda kakae sehemu yako.Unajilizaliza nini hapa?”Vivian alimwachia Denis na kwenda kukaa kwenye kiti chake baada ya kuchimbwa mkwara mzito na askari yule mpelelezi.Kutokana na hali aliyokuwa nayo Denis,ilimhuzunisha kila mmoja aliyekuwa ndani ya chumba kile.Hata wazazi wa Shaimaa walimwonea huruma kaka wa watu kwasababu uso wake ulikuwa umeharibika sana.
Mavazi aliyokuwa amevaa yalichanikachanika katika vurumai lililotokea ndani ya mahabusu.Kutokana na utanashati aliozoeleka kuonekana nao,mtu akimtia machoni kwa muda ule lazima adondoshe chozi bila kutarajia.Mawazo ya Denis yaliamua kutulia ili ajue kitakachoendelea ni nini baada ya ndugu zake pamoja na wazazi wa Shaimaa kufika pale kituoni.
“Hapa haina haja ya kupoteza muda kwasababu tuna kazi kibao za kufanya.Kilichowaleta hapa ni suala la zima la kumtolea dhamana huyu ndugu yenu ili aweze kutoka humu ndani.”Yule askari alianza kuzungumza baada ya hali kuwa shwari.Lakini Brenda,Winfrida pamoja na Vivian bado walikuwa wanalia chini kwa chini pindi walipokutanisha macho yao na uso wa Denis.
“Lakini afande bado hujatueleza Denis kafanya nini mpaka akaletwa hapa?”Dick aliamua kuyakatiza kwanza maelezo ya askari yule ili wajue kosa la Denis hadi akatupwa mahabusu.Alipompigia Dick simu majira ya saa tatu asubuhi,askari huyo alimweleza tu kuwa Dick yupo kituo cha polisi Raskazoni tangu siku iliyopita hivyo afike kwaajili ya kumtolea dhamana.
Baada ya Dick kupata taarifa hiyo alikwenda kuwaeleza wazazi wa Denis ambapo alitumia gari lake dogo kusafiri toka Dar-es-salaam mpaka Tanga akiwa na ndugu wa Denis,mchumba wake pamoja na rafiki yao Dolan.Walifika Tanga saa 10 jioni ambapo waliulizia kituo cha polisi Raskazoni mahali kilipo na baada ya kuelekezwa wlaikwenda moja kwa moja hadi kutuoni hapo kumwona Denis.
Hivyo basi,tangu walipotoka Dar-es-salaam hawakujua Denis kafanya kosa gani mpaka akaingia katika matatizo makubwa kiasi kile.Ndiyo maana Dick akataka kujua kosa lake kabla ya masuala ya dhamana hayajafuata.
“Mnawaona hawa wazee hapa mbele yenu?”Afande alipouliza swali hilo kila mtu alihamishia macho kwa wazazi wa Shaimaa.

“Ndiyo tunawaona.”Wote walijibu kwa pamoja.
                  ********
Itaendelea........Tunaomba radhi kwa kutorusha simulizi hii kwa majuma kadhaa....Hii ilisababishwa na kuharibika kwa kompyuta iliyokuwa inatumika kupostia hadithi.Sasa hivi tumerudi kwa kasi na simulizi itaendelea kama kawaida.Nawatakia siku njema na Mungu awabariki sana.
                ******
Kwa maoni au ushauri napatikana kwa namba 0655089197/0766123623

Share this

Related Posts

Previous
Next Post »