STORY-PENZI LA MSHUMAA
MTUNZI-MZIRAY F.M.
SEHEMU YA 15
Ilipoishia sehemu ya 14
Hivyo basi,tangu walipotoka Dar-es-salaam hawakujua Denis kafanya kosa gani mpaka akaingia katika matatizo makubwa kiasi kile.Ndiyo maana Dick akataka kujua kosa lake kabla ya masuala ya dhamana hayajafuata.
“Mnawaona hawa wazee hapa mbele yenu?”Afande alipouliza swali hilo kila mtu alihamishia macho kwa wazazi wa Shaimaa.
“Ndiyo tunawaona.”Wote walijibu kwa pmaoja.

Sasa endelea..........
“Basi hapo walipo wana huzuni tele baada ya huyu kinyago kumgonga mtoto wao na kumvunja miguu yote.Kwa bahati nzuri alipata kidogo moyo wa huruma na kumbeba huyo binti hadi hospitalini hapo Bombo.Lakini cha kushangaza baada ya kumfikisha hospitali akataka kutoroka na kumsusia msichana wa watu pale Bombo ilihali akiwa katika hali mbaya sana.Basi madaktari kuona vile wakatupigia simu mara moja tufika pale na kumdhibiti.Kama huyo binti atafariki dunia huyu lazima apelekwe mahakamani kwa kesi ya mauaji.”Afande alimaliza kuwaeleza kosa la bandia alilolifanya Denis.Kila mtu aliinamisha kichwa chini kwa masikitiko.
“Sasa ndiyo mumpige kiasi hicho?”Vivian aliropoka baada ya uvumilivu kumshinda.
“Unasemaje we binti?Hebu ngoja,nadhani hujatujua vizuri.Hello!over,over!naomba askari wanne hapo.Haraka sana wafike ofisini kwangu.”Yule afande alikasirishwa sana kwa kitendo cha Vivian kumkaripia kwa sauti ya ukali.
“Hivi we binti una akili timamu?Unasema huyo kapigwa!Umemwona mwanangu alivyosagika miguu yake?Au unadhani sisi wazazi tumelifurahia hilo suala?Kwahiyo ninyi ndiyo mna uchungu sana kuliko huyo mwanetu aliyepewa ulemavu wa kudumu!Sisi ni wazazi wake lazima tuumie kushinda hata ninyi.Mtoto anauma ati!”Mama yake Shaimaa alimcharukia Vivian baada ya kuonesha waziwazi kuumizwa na kitendo alichofanyiwa mchumba wake.
“Mama usiwe na wasiwasi huyu nitamshikisha adabu sasa hivi.”Yule askari alimtuliza Bi Zena kwa kumwambia kuwa atamshughulikia Vivian yeye mwenyewe.Dakika moja mbele mlango wa kile chumba ukafunguliwa na askari wanne wakaingia wakiwa na virungu mkononi.Deni alipoona vile alianza kumwombea msamaha mchumba wake.Aliijua vizuri kazi ya vile virungu maana kibano alichokipata siku iliyopita hakielezeki.
“Afande tafadhali naomba umsamehe huyo binti.Hilo siyo kosa lake ameteleza tu afande.Naomba umsamehe ama kama vipi niadhibu mimi badala yake.”
“Hapana,huyu hawezi kutupangia kazi.Hili ni jeshi la polisi siyo danguro.Kama umezoea kuwa bania pua hao unaowauzia uchi siyo hapa,ni huko huko.Vijana!”Yule askari aliita kwa sauti ya ukali.
“Naam afande.”
“Nataka huyu binti arudi hapa akiwa hatamaniki.”
“Sawa afande.”
“Afande jamani nakuomba umsamehe tu bure.Niadhibu mimi badala yake.Tadhali afande nipo chini ya miguu yako.”Denis alidiriki kudondosha machozi akimwombea Vivian msamaha.Kweli polisi fanya nao masihara wanapokuwa mtaani.Ukishaingia kwenye 18  zao inabidi uwe mpole kama maji mtungini la sivyo utaonja joto ya jiwe.
Hawa jamaa wapinge kwa kutumia sheria lakini siyo kuwaropokea ovyo.Hakika watakutengenezea zengwe ambalo litakuingiza matatizoni mzima mzima.Hata kama utakuja kufanikiwa kulitatua zengwe hilo lakini tayari watakuwa wamekupotezea muda wako na shughuli zako kudorora.Hilo ndilo lililotaka kumkuta Vivian baada ya kuwa mropokaji ndani ya kituo cha polisi.Ni bora uwe mpole kwanza halafu kama utahisi kuwa umeonewa una haki ya kikatiba inayokuruhusu kuwafungulia mashtaka mahakamani.
Malalamiko ya Denis yalimfanya yule afande aligeze kamba. “Haya hebu mwacheni.Nyama wewe!Siku nyingine usirudie kuleta upumbavu wako kwenye kituo cha polisi.Shenzi kabisa,Malaya wa kale wewe!”Denis aliachia tabasamu hafifu baada ya mchumba wake kusamehewa.
“Afande nini kinaendelea hapa?Sisi tunataka tukamtazame mwanetu.”Mzee Kambi aliuliza kinachofuata kwani walikuwa na safari ya kwenda Bombo hospitali kumjulia hali binti yao Shaimaa.
“Tulia mzee wangu tuyamalize sasa hivi.Najua mna uchungu mno juu ya hali ya mtoto wenu.Sasa ni hivi,Dick,si mmekuja kumwombea Denis dhamana?”
“Ndiyo afande.”Dick alijibu kwa unyenyekevu.
“Dhamana tutakupatia bila gharama zozote zile kwasababu ni haki ya mtuhumiwa kupata dhamana.Lakini kutokana na kosa alilolifanya na hali aliyokuwa nayo binti wa hawa wazee kule hospitalini,dhamana hiyo itakuwa na masharti kadhaaa.Je mpo tayari?”Afande aliwauliza akina Dickson.
“Ndiyo tupo tayari.”Dick alijibu kwa niaba ya wenzake.Denis akiwa na pingu zake mkononi aliinua uso wake sambamba na kuyafungua masikio yake ili asikie hayo masharti ya dhamana.Yule askari aliwaangalia wazazi wa Shaimaa kisha akahamishia macho yake kwa ndugu wa Denis.Aliachia tabasamu kisha akalisawazisha koo lake na kuanza kuzungumza.
“Kutokana na kosa alilolifanya bwana mdogo Denis hapa,itabidi awajibike kwa kulipa gharama zote za matibabu ya huyo binti aliyemvunja miguu.Gharama hizo ni za kuanzia jana alipofanya tukio hilo mpaka pale atakapopona.Wakati huo uchunguzi bado ukiendelea kufanyika na kama ikigundulika kuwa Denis hakuhusika na ajali hiyo basi anayo haki ya kufungua kesi ya madai ya fidia mahakamani na atalipwa gharama zake zote alizotoa hospitalini.Sambamba na hilo kila tutakapomhitaji basi afike hapa kituoni kwa wakati.Hayo maelezo niliyowapa yapo kwenye hizi karatasi na kama mkikubaliana nayo mtatia sahihi zenu hapo chini.”
Dick alichukua karatasi moja yenye yale masharti ya dhamana na kuanza kuisoma.Denis naye alipewa ya kwake na baada ya kuisoma aliinua uso wake na kumtazama Dick ambaye naye alikuwa anamwangalia.Wazazi wa Shaimaa baada ya kupitisha macho juu ya karatasi zile walizihamishia kwa akina Brenda ambao nao walisoma na kuridhika.Kilichobaki ilikuwa ni maamuzi tu ya Denis kama atakubaliana na masharti yale ama la!
Moyo wa Denis ulionesha ugumu kidogo juu ya suala lile.Japokuwa alikuwa katika mazingira magumu lakini hakutaka kutwishwa mzigo mkubwa kiasi kile.Siyo kwamba hakuwa na fedha la hasha!Aliamini kuwa anaonewa  kwa kupewa majukumu ambayo hayastahili.
Hivyo basi,Denis alitikisa kichwa kuashiria kutokubaliana na masharti yale.Kila mtu alimshangaa kwani hali aliyokuwa nayo ni mbaya sana na asingestahili kuendelea kukaa ndani. “Denis,kwanini hutaki kukubaliana na hili?Eti afande,tukishasaini hapa si anatoka leo leo.”Dolan ndiyo alishangaa zaidi ya wengine.Hakutarajia kama Denis angekuwa tayari kuendelea kukaa mahabusu.
“Denis,kaka Denis hili suala mbona ni dogo sana kwako!Inamaana utashindwa kumhudumia huyo msichana?Una pesa kiasi gani kaka?Tusaini tu ili uwe huru kwanza,mambo mengine tutayashughulikia ukiwa nje.”Winfrida naye alihamaki baada ya Denis kupingana nao.Brenda na Vivian waliamua kukaa kimya huku wakimwangalia Denis kwa masikitiko.
“Jamani mimi nimeshawaambia kuwa sijamgonga huyo binti.Kwanini nikubali kubeba mzigo ambao siyo wa kwangu!Acheni tu niendelee kukaa humu ndani mpaka siku watakayonipeleka mahakamani.Hiki ni kituo tu cha polisi hawana haki ya kunihukumu kwa lolote lile.Eti nimuhudumie huyo msichana!kwani hawa ni mahakimu?Ushahidi wa kwamba mimi ndiyo nimemgonga upo wapi?Kwa hili siwezi kukubaliana nalo.”
“Denis come on my brother.Sikiliza nikuambie rafiki yangu,tufanye kwanza mpango wa kutoka hapa halafu tutalifuatilia hili suala kwa kina.Chamsingi uwe kwanza huru hayo mengine baadae.”Dick naye hakusita kumsihi rafiki yake akubaliane na yale masharti ili atoke eneo lile.Uzalendo ulimshinda tena Vivian baada ya kumwona mchumba wake akiendelea kung’ang’ania kubaki mahabusu.Aliinuka na kupiga hatua kadhaa mpaka alipomfikia Denis.Alipiga magoti mbele yake na kumkumbatia huku akimwaga machozi kwa uchungu.
“Denis naomba tu ukubaliane na hayo masharti ili utoke hapa.Tazama jinsi ulivyokuwa katika hali mbaya namna hiyo.Umelala tu usiku wa jana,je,ukikaa wiki nzima itakuaje?Unanihuzunisha mno mimi mpenzi wako kila ninapokuona katika hali hiyo.Si mimi tu,tazama ndugu zako Brenda na Winfrida wanavyokulilia.Waangalie marafiki zako Dick na Dolan wanavyohuzunika kwaajili yako.Wazazi wako ndiyo hawana hali kabisa,wapo hoi bin-taaban.Waliposikia habari hizi juu ya matatizo yaliyokupata walilia sana.Sasa tutakwenda kuwaambia nini tukirudi mikono mitupu?Tafadhali nakusihi kubaliana nao,hayo mengine tutafuatilia baadae.”
Ushawishi wa mpenzi huwa na nguvu sana kuliko wa mtu mwingine yeyote yule.Maneno yaliyotoka katika kinywa cha Vivian yalimshambulia Denis na kulainisha moyo wake ambapo aliamua kukubaliana na yale masharti ya dhamana ili aweze kutoka.Baada ya kutia sahihi yake wazazi wa Shaimaa nao walisaini halafu wakakabidhi kwa mashahidi ambao ni Dick,Dolan,Brenda,Winfrida  pamoja na Vivian.Vile vile hata wale askari wengine waliokuwepo mule ndani nao walisaini.
Baada ya zoezi hilo kukamilika,Denis alikabidhiwa baadhi ya vitu vyake na vingine aliambiwa aviache pale kama dhamana.Waling’ang’ania vitambulisho vya kazi pamoja na leseni yake.Vile vile Dick naye aliacha kitambulisho chake kama shahidi wa dhamana.Denis alitolewa nje na kukabidhiwa gari lake ambapo kila mtu alishangaa mno.
“Haaa!kaka Denis ndiyo umenunua hii gari!Duuh!ni noma.”
“Jamani mume wangu,hongera.Tabasamu basi kidogo mpenzi wangu!”
“Denis si utabasamu jamani baby anakuomba.Au unatuonea aibu dada zako?”Brenda aliamua kuvunja ukimya aliokuwa nao kwa muda mrefu.Denis aliachia tabasamu nono na kuwakumbatia wote waliokuja kumtolea dhamana.Kila mmoja alimpa pole kwa yale yaliyomkumba.Baada ya hapo Denis alimkabidhi Dick funguo yake ya gari na kumwambia yeye ndiyo awe dereva.Dick naye alitoa funguo ya gari alilokuja nalo toka Dar-es-salaam na kumrushia Brenda.
Walipomalizana na wale askari,waliwapakia wazazi wa Shaimaa na kuelekea Bombo hospitali.Walipofika ndani ya hospitali hiyo Denis alielekea ndani ya chumba cha daktari.Kwa bahati nzuri hakumkuta yule dokta aliyemchoma kwa polisi siku aliyompeleka Shaimaa pale hospitali.Alifanyiwa mattibabu ya uso wake sambamba na kupewa dawa za kupunguza maumivu ya mwili.Baada ya kutoka kwa dokta hakumkuta mtu mwingine yeyote kwenye benchi la kupumzikia zaidi ya mchumba wake,Vivian.Walitazamana kwa sekunde kadhaa kabla ya kukumbatiana kwa nguvu.
Kila mmoja alivuta hisia za mapenzi kwa mwenzake.Walibembelezana huku wakipapasana migongoni mpaka walipotosheka.Baada ya kuachinana Denis aliuliza watu wengine wapo wapi ndipo Vivian alipomvuta mkono na kmpeleka kwenye hodi aliyolazwa Shaimaa.
Alipoingia ndani ya chumba hicho alikuta kitanda alicholala msichana huyo kikiwa kimezungukwa na wazazi wake pamoja na akina Dick,Dolan na wadogo zake.Denis alipofika tu kila mmoja aligeuka na kumtazama kwa huruma.Alikuwa anachechemea kwa mbali kutokana na kupigwa kwa virungu vya polisi maeneo ya magoti.
Denis alipomtazama Shaimaa hasira zilimkaba akashindwa kuzungumza.Badala yake alimwaga machozi kuyapoza machungu aliyokuwa nayo.Alijiuliza ni kwanini msichana huyo aliamua kumsingizia ajali ambayo hakuhusika nayo.Alishindwa kuelewa ni kipi hasa kilichomfanya Shaimaa kumsukumia yeye mzigo usiokuwa wa kwake.Kutokana na hilo,moyo wake ulimea chuki yenye kutu juu ya msichana yule.
Hakutaka kuonesha waziwazi kuwa anamchukia Shaimaa.Badala yake aliamua kujikaza na kujipa muda ili ajue lengo hasa la msichana huyo kumfanyia udhalilishaji ule.Hakika Denis alishadhalilika sana mbele ya madaktari na manesi wa pale Bombo.Vile vile alipopelekwa polisi alidhalilishwa na askari wa kituo kile pamoja na mahabusu wenzake.Kila alipokumbuka matukio hayo aliumia sana moyoni.

“Basi Denis usilie mpenzi wangu.Haya mambo tutayamaliza tukishatoka hapa.Tutazungumza kwa kirefu na wazazi wa huyu binti tujue tunamalizana vipi nao ili turudi Dar-es-salaam.”Vivian alimfuta Denis machozi na kumwambia akaze moyo yeye ni mtoto wa kiume.Alimshika mkono na kusogea naye karibu na kitanda cha Shaimaa.
                      *********
Itaendelea.....Nashukuru kwa ufuatiliaji wako wa hadithi hii.Nakutakia siku njema na Mungu akujalie afya tele ili uweze kutimiza majukumu yako ya kila siku.
                    *********
Kwa maoni au ushauri napatikana kwa namba 0655089197/0766123623

Share this

Related Posts

Previous
Next Post »